2014-01-11 08:30:30

Majibu ya maswali dodoso kuhusu changamoto za maisha ya ndoa na familia ni kielelezo cha utamaduni wa majadiliano ndani Kanisa


Baraza la Maaskofu Katoliki Uswiss limepata majibu kutoka kwa waamini wapatao 23, 000 waliojibu maswali dodoso yaliyotolewa na Baraza la Kipapa la Familia kama sehemu ya mchakato wa Maandalizi ya Maadhimisho ya Sinodi Maalum ya Maaskofu kuhusu Familia, itakayoadhimishwa mjini Vatican, kuanzia tarehe 5 hadi tarehe 19 Oktoba, 2014. RealAudioMP3

Maaskofu wanasema, majibu kutoka kwa waamini na watu wenye mapenzi mema yamevuka matarajio waliyokuwa nayo mara baada ya kutoa maswali dodoso, kielelezo cha mwanzo wa utamaduni wa majadiliano ya kina kuhusu maswala nyeti ya maisha na utume wa Kanisa ili kujenga na kuimarisha uhusiano mwema na hali ya kuaminiana kati ya waamini na viongozi wa Kanisa

Maswali dodoso yalijikita zaidi na zaidi kuhusu mikakati ya kichungaji kwa wanandoa, tunu msingi za maisha ya kifamilia na changamoto zake; na jinsi ambavyo Kanisa linaweza kuwasaidia wanandoa kutekeleza dhamana na wajibu wao ndani ya Kanisa na Jamii katika ujumla wake.

Waamini wengi nchini Uswiss wanamshukuru na kumpongeza Baba Mtakatifu Francisko kwa kuguswa na mateso pamoja na mahangaiko ya wanandoa sehemu mbali mbali za dunia, kiasi cha kutoa kipaumbele cha kwanza katika utume na maisha yake, jambo linalojionesha kwa kuitisha Sinodi Maalum ya Maaskofu kwa ajili ya Familia na sala kwa ajili ya kuombea Familia.

Waamini wanachangamotishwa na Mama Kanisa kushiriki kikamilifu kujibu maswali dodoso yatakayosaidia kutengeneza hati ya kutendea kazi wakati wa Maadhimisho ya Sinodi ya Maaskofu kwa ajili ya Familia, ijulikanayo kwa lugha ya Kilatini kama “Instrumentum Laboris”.








All the contents on this site are copyrighted ©.