Changamoto za kichungaji baada ya Maadhimisho ya Mwaka wa Imani
Bwana tuongezee imani, ndiyo kauli mbiu inayoongoza barua ya kichungaji ya Patriaki
Fouad Twal wa Yerusaleme katika kufunga Mwaka wa Imani, uliotangazwa na kuzinduliwa
na Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI, ukaendelezwa na hatimaye kufungwa rasmi na
Papa Francisko kwa kishindo kikubwa, sanjari na Maadhimisho ya Sherehe za Kristo Mfalme
wa Ulimwengu.
Mwaka wa Imani
kimekuwa ni kipindi ambacho kimetoa changamoto kwa waamini kukiri, kuadhimisha, kuishi
na kushirikisha wengine Furaha ya Injili.
Ni mwaka ambao uliosheheni matukio
makubwa katika maisha na utume wa Kanisa. Ni mwaka ambao umeshuhudia Baba Mtakatifu
Benedikto wa kumi na sita aking’atuka kutoka madarakani kwa utashi kamili na kwa ajili
ya ustawi na maendeleo ya Kanisa la Kristo. Familia ya Mungu ikashuhudia Papa Francisko,
mtu wa watu akichaguliwa kuliongoza Kanisa kama Khalifa wa Mtakatifu Petro; kiongozi
anayeendelea kuwashangaza wengi kutokana na unyenyekevu na mikakati yake ya kichungaji
inayotoa kipaumbele cha kwanza kwa: Mungu, Kristo, Kanisa na binadamu aliyeumbwa kwa
sura na mfano wa Mungu.
Baba Mtakatifu Francisko ni kiongozi anayeonesha cheche
za mwendelezo wa mageuzi ndani ya Kanisa, ili kufikia utimilifu wa maisha ya Kikristo,
yaani utakatifu. Mlango wa Imani, Mwanga wa Imani na Injili ya Furaha ni nyaraka ambazo
zina umuhimu wa pekee katika maisha na utume wa Kanisa, lakini kwa namna ya pekee,
katika mchakato wa Uinjilishaji Mpya unaojikita katika imani tendaji inayotolewa ushuhuda
na waamini katika uhalisia wa maisha.
Patriaki Twal anasema kwamba, imani ni
fadhila ya Kimungu ambayo kwayo waamini wanamsadiki Mungu na kila kitu alichokisema,
alichofunulia, na ambacho Kanisa Takatifu linawataka waamini kusadiki, kwa sababu
Mungu ndiye kiini cha ukweli wenyewe. Imani ni mwanga angavu unaowangazia mwamini
ili asitembee katika dhambi na uvuli wa mauti. Imani inamwezesha mwamini kufanya maamuzi
ya busara kwa wakati muafaka pamoja na kuendelea kutambua mapenzi ya Mungu. Hii ni
zawadi na nguvu kutoka kwa Mwenyezi Mungu, ili kutekeleza utashi wake.
Imani
ni hazina kubwa kwa waamini wanaoishi katika Nchi Takatifu, kwani wao wamebahatika
kuishi katika maeneo Yesu amezaliwa, ameishi, akateswa, akafa na kufufuka kutoka katika
wafu ili kukamilisha kazi ya Ukombozi. Waamini wanapaswa kuwa ni mashahidi amini wa
Kristo Mfufuka pasi na woga, hata kama wanaonekana kuwa ni kundi dogo, katika Nchi
Takatifu.
Waamini wanakumbushwa kwamba, Mwenyezi Mungu ni mwaminifu kwa ahadi
zake, changamoto kwa waamini pia kuwa waaminifu kwa Mwenyezi Mungu kama inavyojionesha
katika Maandiko Matakatifu, lakini kwa namna ya pekee kwa Mzee Ibrahim, Baba wa Imani
kamilifu, aliyejiachilia mikononi mwa tunza na ulinzi wa Mwenyezi Mungu katika mapito
ya maisha yake.
Patriaki Twal anasema, imani inajionesha kwa namna ya pekee
katika maisha ya Bikira Maria, aliyejitahidi kumwilisha imani katika matendo ya huruma
kama inavyojionesha alipotoka kwa haraka kwenda kumhudumia binamu yake Elizabeth aliyekuwa
mjamzito; walipolazimika kukimbilia nchini Misri ili kuokoa maisha ya Mtoto Yesu,
aliposimama chini ya Msalaba akamwona Mwanaye wa pekee akiinamisha kichwa na kukata
roho kwa ajili ya ukombozi wa mwanadamu.
Bikira Maria ni kielelezo cha imani
thabiti, inayomkirimia mwamini amani, utulivu wa ndani na utakatifu wa maisha. Kimsingi
anasema Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita, imani inapaswa kujionesha
katika matendo ya upendo ili kudumisha matumaini pasi na kukata tamaa.
Wakristo
katika Nchi Takatifu wanakabiliana na hali ngumu ya maisha, wasi wasi na hata wakati
mwingine wanaonja dalili za kukata tama. Waamini wanakumbushwa kwamba, Mwenyezi Mungu
kwa njia ya Mwanaye Yesu Kristo atawafariji kwa njia ya imani, matumaini na mapendo.
Patriaki
Twal anawaambia Wakristo kwamba, haitoshi kuzaliwa na kukulia katika Familia ya Kikristo,
bali neema hii inapaswa kuendelezwa kwa kukubali kukutana na kumpokea Neno wa Mungu
aliyefanyika mwili kwa ajili ya ukombozi wa mwanadamu, akawapatia neema ya kufanyika
watoto wateul wa Mungu, changamoto ya kuendelea kumtolea ushuhuda wa maisha, kwa kuwaonjesha
wengine Injili ya Furaha; Huruma na Upendo; kwa kusimama kidete kulinda na kutetea
haki msingi za binadamu. Ni mwaliko wa kulinda na kutunza mazingira kwani hii pia
ni sehemu ya kazi ya Uumbaji ambayo inaimba sifa ya matendo makuu ya Mungu.
Wakristo
wanakumbushwa kwamba, Yesu Kristo ni Neno wa Mungu aliyefanyika mwili, katika mambo
yote akawa sawa na binadamu ila hakutenda dhambi. Yesu Kristo amewafunuliwa watu sura
ya Mungu inayojikita katika huruma na mapendo. Ni Bwana na Mwalimu aliyeonesha umabhiri
wake katika Heri za Mlimani na kwenye Sala ya Baba Yetu. Ni mwaliko kwa waamini kuwa
ni Kristo mwingine, ili watu waweze kuguswa na ushuhuda wa imani inayomwilishwa katika
matendo! Tafakari ya Fumbo la Umwilisho linalopata hitimisho lake katika Fumbo la
Pasakaa, hii ni fursa fursa ya kuona matendo makuu ya Mungu katika kazi ya Uumbaji
na Ukombozi.
Kwa Wakristo, Yesu ni Mkombozi; ni Neno wa Mungu na sura ya Baba
wa Milele, changamoto kwa waamini kujitaabisha kumfahamu, kumpenda na kumtumikia Kristo,
ili awasaidie kuwaongoa na hatimaye, kuwawezesha kuwa ni watu wapya zaidi. Yesu ni
mpole na mnyenyekevu wa moyo; ni kielelezo cha Mtumishi mwaminifu, aliyethubutu kuyamimina
maisha yake kwa ajili ya rafiki zake. Wakristo wakipenda wanaweza kufanya tafakari
ya kina kuhusu maisha na utume wa Yesu unaosimuliwa kwa namna ya pekee katika Maandiko
Matakatifu.
Biblia ni maktaba kubwa kuliko zote ulimwenguni, ina vitabu 46
vya Agano la Kale na Vitabu 27 kutoka katika Agano Jipya, waamini wajitaabishe kulisoma,
kutafakari na kumwilisha Neno la Mungu katika uhalisia wa maisha. Neno la Mungu ni
dawa ya maisha ya kiroho, ni shule ya utakatifu wa maisha na ukombozi wa mwanadamu.
Patriaki
Twal katika barua yake ya kichungaji kama sehemu ya kufunga Mwaka wa Imani, anawakumbusha
waamini kwamba, wanasukumwa kuamini katika Kanisa moja, takatifu, katoliki na la mitume.
Hii ndiyo imani ambayo Mitume wameirithisha kwa waamini vizazi baada ya vizazi, changamoto
kwa waamini kwa njia ya imani, kuchuchumilia utakatifu wa maisha, kwa toba na wongofu
wa ndani. Watakatifu ni mifano bora ya kuigwa katika imani na nguzo rejea katika hija
ya maisha ya hapa duniani. Hata leo bado kuna watakatifu wanaoendelea kutolea ushuhuda
wa imani ka Kristo na Kanisa lake, sehemu mbali mbali za dunia.
Patriaki Twal
anawaalika Wakristo kutolea ushuhuda wa imani yao kwa Kristo na Kanisa lake, kwa kutambua
kwamba, kwa njia ya Sakramenti ya Ubatizo, kila Mkristo amepewa dhamana ya kuwa ni
Mmissionari, tayari kujitosa kimasomaso kutangaza Habari Njema ya Wokovu hadi miisho
ya dunia. Hii ni imani inayojisimika katika Fumbo la Utatu Mtakatifu, Kanisa na Mambo
ya Nyakati.
Familia, Parokia na shule ziwe ni mahali pakutangaza na kurithisha,
kukuza na kukomaza imani kwa njia ya: Neno la Mungu, Sakramenti za Kanisa na Matendo
ya huruma. Mapadre na Watawa wanahamasishwa na Mama Kanisa kuwaimarisha ndugu zao
katika imani, matumaini na mapendo, kwa kutambua kwamba, wao ni Wamissionari wenye
dhamana ya kumhubiri Kristo hadi miisho ya dunia. Mara baada ya Maadhimisho ya Mwaka
wa Imani, Kanisa bado lina dhamana na utume wa kuendelea kutangaza Injili ya Furaha
hadi miisho ya dunia.
Patriaki Twal anasema, tangu mwanzo damu ya mashahidi
na wafiadini imekuwa ni mbegu ya Ukristo sehemu mbali mbali za dunia, hata leo hii
bado kuna watu wanateseka kutokana na imani yao kwa Kristo na Kanisa lake. Hii ni
kutokana na misimamo mikali ya kiimani na baadhi ya watu kukosa utamaduni wa kuvumiliana.
Wakristo kama raia wengine katika Nchi Takatifu wana haki ya kuishi hapa. Wakristo
wajiandae kutoa sadaka hata ikibidi sadaka ya maisha yao, kama inavyoendelea kujitokeza
sehemu mbali mbali huko Mashariki ya Kati.
Wakristo wanaalikwa kujitokeza kifua
mbele ili kushiriki kikamilifu katika maisha ya hadhara na wala hakuna sababu ya kujitenga,
kwani kuishi katika Nchi Takatifu ni neema na baraka na wala si laana. Wawe ni mashahidi
amini wa Yesu Kristo Bwana na Mwalimu; kwa kutambua kwamba, wanayo dhamana ya kushiriki
katika maisha na utume wa Kanisa, tayari kutolea ushuhuda wa hazina kubwa ya imani
wanayoibeba katika mioyo yao!
Patriaki Fouad Twal wa Yerusalem anahitimisha
Barua yake ya kichungaji kama sehemu ya mchakato wa kufunga Mwaka wa Imani kwa kuwataka
waamini na watu wote wenye mapenzi mema kuimarisha matumaini yao kwa Kristo na Kanisa
lake; kwa kutolea ushuhuda wa imani tendaji sanjari na kutambua umuhimu wa imani katika
maisha na utume wa Kanisa.
Maisha ya Mkristo yaendelee kutoa harufu ya utakatifu
wa maisha, kwa njia ya toba na wongofu wa ndani; kwa kusimama kidete kulinda na kutetea
misingi ya haki, amani, utulivu; maisha, utu na heshima ya binadamu. Waamini wawe
ni mashahidi amini wa imani, matumaini na mapendo, kiasi hata cha kuyamimina maisha
yao kwa ajili ya Kristo na Kanisa lake.
Kwa njia ya neema na baraka za Mwenyezi
Mungu, Wakristo washinde kishawishi cha kutaka kuikimbia Nchi Takatifu kwa kuogopa
madhulumu, bali waendelee kuwa ni chumvi na mwanga wa mataifa, hata katika uchache
na udogo wao kama Jumuiya ya waamini. Kamwe wasikose kumwomba Yesu Kristo awaongezee
imani.
Barua hii ya kichungaji imehaririwa na Padre Richard A. Mjigwa,
C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.