Ufunguzi wa Mwaka wa Masomo Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustino cha Tanzania kwa Mwaka
2013-2014 lilikuwa ni tukio ambalo lilileta mvuto na mguso kwa wanafunzi wapya wanaoanza
safari ya masomo yao Chuoni hapo.
Kila Mkuu
wa kitivo, alipata nafasi ya kunadi na kuwatambulisha wadau mbali mbali watakaoshirikiana
nao katika kunoa akili na kujipatia maarifa kutoka katika Chuo Kikuu cha SAUT, ambacho
kwa sasa kinaendelea kupata mafanikio makubwa ndani na nje ya Tanzania.
Kwa
ujumla wanafunzi walichangamotishwa na wakuu wa vitivo kuhakikisha kwamba, wanajenga
utamaduni wa kujisomea ili kujifunza zaidi, huku wakizingatia rasilimali muda na kwamba,
wapaswa kuonesha bidii na nidhamu ya kutaka kujipatia elimu, maarifa na ujuzi katika
maisha yao Chuoni hapo.
Katika mchakato wa kujipatia elimu, watambue kwamba,
kuna changamoto kubwa ambazo ziko mbele yao: hizi ni changamoto za ujana na uzee na
kwamba, wanapaswa kujenga imani na matumaini kwa kile wanachokifanya. Chuo kikuu ni
mahali ambapo wanapaswa pia kujifunza kuishi na wengine kama Jumuiya ya Wasomi, wakitambua
kwamba, wanapaswa kushiriki kikamilifu katika maisha na utume wa SAUT. Umefika wakati
kwa wanafunzi kuacha visingizio visivyo na tija wala mashiko kwa maisha yao kama wanafunzi.
SAUT inaendelea kuboresha mitandao ya mawasiliano ili kuwapatia fursa ya kuweza kujifunza
zaidi.
Hapa anasema Padre Thaddeus Mkamwa, Kaimu Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu
cha SAUT, taaluma kwamba, wanafunzi wanapaswa kujikita katika masomo na kuacha kupepeta
mdomo! Waachane na matumizi mabaya ya mitandao na badala yake wajenge tabia ya kuwajibika
zaidi wakitambua sadaka na majitoleo yanayofanywa na wadau mbali mbali katika mchakato
wa kuhakikisha kwamba, wanapata elimu bora wawapo Chuoni hapo.
Vitivo mbali
mbali vilivyoko SAUT vimepata mafanikio makubwa katika kipindi cha Mwaka wa Masomo
2012-2013. Haya ni mafanikio yaliyojionesha katika ngazi ya kitaifa na kimataifa.
Kitivo cha sheria, mawasiliano ya jamii, elimu, biashara na uandisi ni kati ya vitivo
ambavyo vinaendelea kufanya vyema zaidi. Kwa mfano kitivo cha sayansi ya mawasiliano
ya Jamii, kimeendelea kuzalisha waandishi wa habari wanaotegemewa ndani na nje ya
Tanzania kutokana na umakini, weledi, nidhamu na majitoleo yao wanapokuwa katika uwanja
wa habari na mawasiliano. Hili ni jambo la kujivunia! Mafanikio kama haya yanajionesha
pia katika kitivo cha elimu, ambacho ni kati ya vitivo vikongwe SAUT.
Wahadhili
wa Chuo Kikuu cha SAUT wanaendelea kuhamasishwa kufanya tafiti na kuzichapisha kwa
ajili ya mafao ya wasomi na Jamii kwa ujumla. Kitivo cha usimamizi wa biashara kimeendelea
kuwaandaa wanafunzi kutoka SAUT katika ulimwengu wa kazi na ajira. Kinaendelea kuwekeza
katika sekta ya utalii ili kuwajengea wanafunzi uwezo wa kutoa huduma bora, kwa kuimarisha
utamaduni wa kushirikiana, kila mtu akijitahidi kutumia vyema karama na vipaji alivyokirimiwa
na Roho Mtakatifu. Wanafunzi wa SAUT wanakumbushwa kwamba, hapo ni mahali pa kujenga
na kuimarisha mapaji ya Roho Mtakatifu kwa ajili ya mafao ya wengi.
Kitivo
cha uhandisi ni kati ya vitivo vichanga kabisa kwenye Chuo Kikuu cha SAUT, lakini
kinapania kuhakikisha kwamba, kinachangia kwa kiasi kikubwa kuzalisha wahandisi watakaoshiriki
katika kuleta ufumbuzi wa ukosefu wa wahandisi nchini Tanzania, jambo ambalo kwa sasa
linaonekana kuwa kama “janga la kitaifa”. Takwimu zinaonesha kwamba, tangu Tanzania
iliojipatia uhuru wake kutoka kwa Mwingereza kunako mwaka 1961 imefanikiwa kuandaa
waandisi 13,000 tu.
Lengo la taifa lilikuwa ni kuwandaa wahandisi 80,000,
jambo ambalo bado halijafikiwa. Wengi walioandaliwa wamekimbilia nje ya nchi ili kutafuta
“malisho bora zaidi” na wachache waliopo wanaendelea kuzeeka na kung’atuka! Kitivo
cha uandisi kitaendelea kuwekeza zaidi katika sekta hii kwani wahitimu wake wana uhakika
wa kupata fursa za ajira. Hiki ni kitengo ambacho hakuna mgomo wa kazi, kumbe SAUT
inaweza kuchangia kwa kiasi kikubwa katika kukabiliana na “janga la ukosefu wa wahandisi
Tanzania”
Kwa ufupi haya ndiyo yaliyojiri katika ufunguzi wa Mwaka wa Masomo,
2013-2014 Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustino cha Tanzania, SAUT, hivi karibuni Jijini
Mwanza. Tukio ambalo lilitanguliwa na Ibada ya Misa Takatifu iliyoongozwa na Dr. Respicius
Rugemalira, Mwanasheria mkuu wa SAUT na baadaye wakuu wa vitivo wakajinadi kwa sera,
mikakati na matarajio yao kwa siku za usoni.
Kutoka SAUT, Jijini Mwanza ni Padre
Richard A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.