2014-01-07 08:37:17

Msipotoshe maneno ya Papa Francisko kuhusu ndoa za watu wa jinsia moja! Watoto wanahitaji malezi ya Baba na Mama!


Padre Federico Lombardi msemaji mkuu wa Vatican anabainisha kwamba, kuna baadhi ya vyombo vya habari nchini Italia vinavyopotosha kwa makusudi kuhusu maoni yaliyotolewa na Baba Mtakatifu Francisko wakati alipokuwa anazungumza na viongozi wakuu wa Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume, hapo tarehe 29 Novemba 2013 kuhusu changamoto za malezi kwa watoto na vijana wa kizazi kipya, tofauti kabisa na miaka kadhaa iliyopita!

Baba Mtakatifu aliwaambia wakuu wa Mashirika kwamba, Familia nyingi kwa sasa zinakabiliana na changamoto nyingi kwani: kuna wazazi waliotengana; kuna ndoa za watu wa jinsia moja, mambo ambayo hayakuwepo kwa miaka kadhaa iliyopita. Elimu, malezi na urithishaji wa imani hauna budi kuzingatia changamoto hizi kwa ajili ya mafao ya vijana wa kizazi kipya; wanaopaswa kusindikizwa kwa busara ya hali ya juu mintarafu hali na mazingira ya familia wanamotoka, ili hata wao, waweze kupokea zawadi ya imani katika mwelekeo chanya!

Padre Federico Lombardi anasema, maoni haya ya Baba Mtakatifu yanagusia dhamana na utume wa Kanisa katika masuala ya elimu na malezi katika ujumla wake na wala si mwelekeo wa Baba Mtakatifu Francisko wa kutaka "kupigia debe" ndoa za watu wa jinsia moja kama ambavyo baadhi ya vyombo vya habari nchini Italia vinavyotaka kuwasadikisha watu.

Baba Mtakatifu alitolea mfano wa mtoto ambaye alijikuta akiwa ameelemewa na huzuni kutokana na ukweli kwamba, mchumba wa mama yake alikuwa hampendi. Haya ndiyo mateso na mahangaiko wanayokabiliana nayo watoto katika maisha ya ndoa na familia. Waamini na watu wenye mapenzi mema, wawe makini kwani kuna watu kwa makusudi mazima wanataka kupotosha ukweli kwa ajili ya mafao yao binafsi. Watoto wanahitaji malezi ya baba na mama kadiri ya mpango wa Mungu katika maisha na mwanadamu!







All the contents on this site are copyrighted ©.