2014-01-07 07:52:50

Anzeni Mwaka Mpya wa 2014 kwa kuwa na maisha mapya yanayosimikwa katika misingi ya imani, matumaini na mapendo!


Baraza la Maaskofu Katoliki Ufilippine katika salam zake za Mwaka Mpya wa 2014, linawaalika waamini kutubu na kuongoka, ili kuachana na maisha ya zamani, tayari kuuanza Mwaka Mpya kwa maisha yanayosimikwa katika imani, matumaini na mapendo; fadhila ambazo zinapaswa kujionesha katika uhalisia wa maisha ya kila siku. RealAudioMP3

Askofu mkuu Socrates Villegas wa Jimbo kuu la Lingayen- Dagupan ambaye pia ni Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Ufilippini anasema, kuna haja kwa waamini na watu wote wenye mapenzi mema kujikita katika toba na wongofu wa ndani, ili kuuvua utu wa kale uliochakaa kutokana na rushwa pamoja na uvunjifu wa misingi ya haki, amani na utulivu.

Umefika wakati kwa wananchi wa Ufilippini kuondokana na tabia ya kuteka watu nyara, kujikita katika vitendo vya kigaidi na rushwa; mambo ambayo kimsingi yanahatarisha amani, ustawi na maendeleo ya wananchi wa Ufilippini ambao kwa sasa wanakabiliana na changamoto nyingi za maisha!

Askofu mkuu Villegas anawatakia waamini na watu wote wenye mapenzi mema, Mwaka Mpya wa 2014, ili uwe ni mwanzo wa maisha mapya yanayosimikwa katika haki, amani, upendo na upatanisho wa kitaifa. Kanisa nchini Ufilippini linasali kwa ajili ya kuombea amani nchini Syria, ili wananchi waweze kupata ujasiri wa kujipatanisha na Mungu pamoja na ndugu zao. Wanasali na kuwaombea wananchi wa Ufilippini walioathirika na tufani iliyotokea hivi karibuni nchini mwao, ili waweze kupiga moyo konde na kupata ujasiri wa kuanza upya tena, kuchakarika ili kujiletea maendeleo zaidi.

Mwaka Mpya ni Siku ya Kuombea Amani Duniani. Ni Siku ya kuombea mshikamano wa kimataifa dhidi ya baa la njaa, ujinga na umaskini sehemu mbali mbali duniani. Ni muda wa kusali na kuombea amani, utulivu na maendeleo ya wengi, huku watu wakijitahidi kukumbatia huruma na upendo wa Mungu unaojionesha kwa njia ya Yesu Kristo aliyemwaga damu yake azizi kwa ajili ya ukombozi wa mwanadamu.

Baraza la Maaskofu Katoliki Ufilippini linawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema, kuanza Mwaka Mpya wa 2014 kwa imani, matumaini na mapendo kwa Mungu na Jirani. Watu wamtangulize Mungu katika maisha na mipango yao, ili waweze kuonja upendo na huruma kwa waja wake. Waamini wasisite kukimbilia ulinzi na tunza ya Bikira Maria Mama wa Mungu.

Waamini wasimame kidete kulinda, kutetea na kushuhudia Injili ya Uhai, dhidi ya utamaduni wa kifo, kama njia ya kumuenzi Bikira Maria aliyekubali kuwa ni Tabernakulo ya kwanza ya Neno wa Mungu aliyefanyika Mwili, akawa mwanadamu katika mambo yote isipokuwa hakutenda dhambi. Yesu ni Mungu kweli na mtu kweli! Huu ni mwaliko kwa kila mwamini pia kutengeneza mazingira katika maisha yake, ili Yesu aweze kupata makao ya kudumu; daima wakiwa tayari kumsikiliza na kutii amri na maagizo yake.








All the contents on this site are copyrighted ©.