Wabunge Kenya wanapania kujenga nyumba kwa ajili ya Mapadre waliostaafu!
Wabunge kutoka Kanisa Katoliki pamoja na waamini wenye mapenzi mema nchini Kenya,
wameanza kujipanga kutekeleza azma ya kujenga nyumba kwa ajili ya Mapadre wazee, ili
waweze kumalizia maisha yao katika hali ya heshima baada ya kujitoa bila ya kujibakiza
kwa ajili ya Kanisa na jirani zao katika huduma ya: Neno la Mungu, Sakramenti za Kanisa
na maisha kwa ujumla.
Wazo hili limejitokeza nchini Kenya baada ya kuwaona
baadhi ya Mapadre katika maisha yao ya uzee wakiteseka, kwa kukosa mahali pazuri pa
kuishi na huduma bora zaidi katika maisha ya uzeeni. Ni changamoto iliyotolewa na
Bwana Thomas Mwadeghu, Mbunge wa Wundanyi, Kenya.
Tayari wamekwisha pata eneo
la ujenzi wa nyumba kwa ajili ya makazi ya Mapadre waliostaafu utume wao na kwamba,
ujenzi unatarajiwa kuanza mwaka 2015 baada ya kukamilisha taratibu zote, kadiri ya
taarifa iliyotolewa na Shirika la Habari la CISA.