Siku kuu ya Tokeo la Bwana, yaani Epifania ni kati ya Sherehe kubwa zinazoadhimishwa
na Mama Kanisa katika Liturujia ya Mwaka wa Kanisa. Mtoto Yesu aliyezaliwa na Bikira
Maria anajifunua kwa mataifa kama Mwana wa Mungu, Masiha na Mwaga wa Mataifa.
Mama Kanisa
katika Maadhimisho ya Siku kuu ya Tokeo la Bwana, anatangaza pia Fumbo la Pasaka,
linaloonesha kwa namna ya pekee, utukufu wa Kristo kati ya watu wake hadi pale atakapokuja
tena kuwahukumu wazima na wafu. Katika hija ya maisha ya kila siku, waamini wanajitahidi
kumwilisha Fumbo la Ukombozi, kiini cha maadhimisho haya ni Liturujia ya Mwaka wa
Kanisa, lakini kwa namna ya pekee, Siku kuu tatu zinazoonesha: mateso, kifo na ufufuko
wa Kristo kutoka katika wafu, yaani Siku kuu ya Pasaka ambayo kwa Mwaka huu itaadhimishwa
hapo tarehe 20 Aprili 2014.
Kila Jumapili, Mama Kanisa anaadhimisha Pasaka
ya Bwana na kuwawezesha waamini kuendelea kuadhimisha tukio hili kuu katika maisha
na imani yao; kwani Kristo ameshinda dhambi na mauti. Siku kuu ya Pasaka ni chemchemi
ya Siku kuu nyingine zote zinazoadhimishwa na Mama Kanisa. Kipindi cha Kwaresima kwa
mwaka huu, kitaanza rasmi tarehe 5 Mwezi Machi 2014 kwa kupakwa majivu, mwaliko wa
toba na wongofu wa ndani.
Mama Kanisa ataadhimisha Siku kuu ya Kupaa Bwana
Mbinguni hapo tarehe Mosi, Juni 2014 na Pentekoste, Siku kuu ya kuzaliwa kwa Kanisa
itaadhimishwa hapo tarehe 8 Juni 2014. Jumapili ya kwanza ya Majilio ambayo kimsingi
ni mwanzo wa Mwaka Mpya wa Kanisa, na maandalizi ya ujio wa Kristo itaadhimishwa hapo
tarehe 30 Novemba 2014.
Mama Kanisa anayeendelea kufanya hija yake hapa duniani
anatangaza pia Pasaka ya Bwana, anapoadhimisha Siku kuu za Bikira Maria Mama wa Mungu
na Kanisa; Siku kuu za Mitume na Watakatifu mbali mbali; anapowakumbuka watoto wake
waliotangulia katika usingizi wa amani, wakiwa na tumaini katika ufufuko wa wafu.
Sifa
na utukufu kwa Kristo aliyekuwepo, aliyepo na atakayekuja. Yeye ni Bwana wa Historia
na nyakati zote ni zake. Amina.