2014-01-04 15:45:27

Epifania ya Bwana: Dhahabu, Uvumba na Manemane! Kazi kwako!


Sikukuu ya Epifania inayoitwa pia Tokeo la Bwana ni sherehe kubwa sana kwa wakristu. Kwa bahati mbaya siku hii imegeuzwa kuwa kama ya maigizo ya watoto wanaopita kuimba nyumba hadi nyumba na kupata zawadi. Kwa hiyo badala ya kuwa Epifania tungeweza kuiita kwa kiingereza Happy-funny. RealAudioMP3

Sikukuu ya leo inayo mafundisho ya maisha yanayoweza kumtosha kila mtu. Ukifaulu kutanguzana kidhati na wasafriri wanaotajwa katika sikukuu ya leo watakufikisha kwenye uhondo wa maisha. Wasafiri hao wanaitwa majusi. Wametokea mashariki ya mbali wakielekea Betlehemu. Wasafiri hao hawatajwi idadi wala majina kama tunavyosadikishwa kuwa walikuwa watatu. Tunaambiwa tu Kulikuwa majusi kutoka mashariki ya mbali.

Msafiri yeyote ni mtu wa kuja siyo mwenyeji, ndiyo maana anaitwa “Msafiri kafiri.” Kama wewe ni msafiri tu hapa duniani, basi hata wewe ni kafiri. Wasafiri wenzako, yaani majusi hawakutembea mikono mitupu, walichukulia tunu au zawadi. Tunu hizo zilikuja kutambulika mwishoni mwa safari yao tena baada ya kumwona mototo Yesu na mama yake, ndipo tunaambiwa, wakatoa tunu zao yaani dhahabu, ubani na manemane. Kutokana na aina ya zawadi walizobeba tunaweza kujua huyu mtoto waliyemtembelea alikuwa wa aina gani.

Kwa mantiki hiyo, katika msafara wa maisha yetu hapa duniani, kila mmoja ni kama tunu au zawadi za kumkabidhi Mungu sasa hivi na hata baada ya maisha ya hapa duniani. Hebu tujaribu kuzitafakari tunu hizo walizozibeba wasafiri wenzetu na tujitafakari sisi wenyewe.

DHAHABU: Ni kito au jiwe la thamani sana. Uthamani wake upo katika uzito wake, uimara, kudumu, uzuri na kupendeza kwake katika kung’aa, dhahabu haipati kutu na wala haichujuki. Watu wengi wameteseka, kuitafuta kwa udi na uvumba pengine hadi kufa. Wewe fuatilia tu vituko vilivyo kwenye machimbo. Mwenye dhahabu ni mtu tajiri sana, hata mfumo wa thamani ya fedha unapimwa kutokana na kiwango cha dhahabu.

Dhahabu ni jiwe asilia lililogeuzwa hali yake kwa kuunguzwa kwa moto mkali sana ulioko ardhini uitwao volcano. Hiyo ni kazi ya huluka (nature), yaani, Mungu ameficha raslimali ndani ya tumbo la mama ardhi. Kwa hiyo utafutaji na uchimbaji wa dhahabu unaonesha thamani ambayo Mungu ameihifadhi kwenye udongo kwa miaka elfu nyingi. Kadhalika hali ya kumtafuta Mungu katika imani. Kwa vile imani inayo thamani zaidi ya dhahabu watu wamepigania kuipata, watu wamefia imani yao kama wachimbaji wadogowadogo wanaofukiwa kwenye migodi.

Baada ya kuichimbua ikiwa katika hali ya udongo yabidi kuihakikisha kama kweli ni dhahabu kwani “si kila king’aacho ni dhahabu”. Masonara hufanya hivyo kwa kuiunguza kwenye jiko (tanuru) la moto wenye joto la selsius elfu moja mia mbili. Kwa kawaida ukiunguza tani moja ya udongo wa dhahabu unapata gram 2 tu za dhahabu.

Kishapo vyembevyembe vya dhahabu iliyosafishwa hufinyangwa kulingana na ukubwa wa kikombola chenye umbo kama la tofali dogo. Hapa ndipo dhahabu inapozidisha thamani yake. Hatua hii ya kusafishwa inaitwa pia kujaribiwa dhahabu, nayo inalinganishwa na mateso anayopata mtu katika maisha ya imani. [Jiko la kuunguza almasi linaitwa Kalibu, na jiko la dhahabu linaitwa tanuru, lakini tanuru la kuunguza moyo wa mtu ni Mungu mwenyewe: “Kalibuni kwa fedha na tanuru kwa dhahabu bali Bwana huijaribu mioyo”(Methali 17:3)].

Wayahudi waliyachukua mateso waliyokuwa wanayapata kuwa ni kujaribiwa. Daima wapatapo mateso, yawe ya vita, au kuchukuliwa utumwa walikuwa wanasali “ Ee Mungu umetujaribu kama dhahabu katika tanuru.” (Hekima 3:6-9); Mungu atupatia mateso ili kutusafisha.

Ndugu yangu, ni kweli kwamba kuwa na imani ya dini yako ndiyo dhahabu yako hiyo. Lakini huko ni sawa na kuwa na dhahabu iliyochanganyika na udongo, bado unahitaji kujaribiwa katika tanuru la mateso ili kutakaswa na kuwa imara na thabiti. Kazi ngumu ya masonara ni ya kuiunguza dhahabu katika tanuru la moto mkali hadi inang’aa. Sisi pia tunahitaji sonara – au shule – ili dhahabu –imani – ijaribiwe.

Kwa mateso imani utaing’arisha na itapendwa na kufuatwa.”Kibaya chajitembeza, chema chajiuza chenyewe”. Mkristo mwenye imani iliyotakaswa ni yule anayejiaminisha, anayejisadikisha mwenye "conviction" – katika kila hali ya maisha. Bahati mbaya siku hizi imani hiyo imegeuka kuwa imani ya kwenye mikutano, imani ya mapambano, ya mikataba, ya kushawishiana, imani hiyo ni dhahabu feki hata kama inang’aa “Kwani si kila king’aacho ni dhahabu.” Tunahitaji mtu mwenye imani thabiti, mkakamavu mwenye kujizatiti. Katika kipengee hicho, ninamwombeni radhi nikisema: “Ashakum si matusi” kwamba wakristu wengi hatujakomaa kiimani.

Tuko bado watoto wadogo kwa vile hatujaisafisha imani yetu katika tanuru la moto mkali wa dhahabu. Mathalani bado hatulielewi Neno la Mungu. Kama tunaelewa basi labda ni kile kidogo tulichojifunza kabla ya kupata komunio ya kwanza, au pengine kwenye mahubiri ya padre siku ya dominika kama naye ameamka vizuri. Kutokana na kutojaribiwa huko, wakati mwingine unapata picha kwamba wakristu wana woga wa kuienjilisha imani yao kwa matendo. Ili kuwa mkristo leo yabidi kuwa shujaa, imara, thabiti mwenye kuweza kujikabili katika imani hiyo, hasa katika matatizo ya maisha.

Takataka nyingi sana zimejinasa kabisa katika dhahabu ya imani yetu, tunabaki kuwa tu na nia njema ya kujilaumu lakini bila kuwa na nguvu ya kujinasua kwa kujisafisha katika tanuru la moto wa majitoleo. Mathalani uchafu mzito wa rushwa ulionasa vibaya katika maisha yetu. Mkristu anajua kabisa kwamba “Mungu wetu si Mungu wa Rushwa”. Kwa nini basi usianze wewe kujitia katika tanuru hilo la moto la kusafisha. Huko ndiko kuwa dhahabu, iliyojaribiwa na ikawa dhahabu hai inayompendeza Mungu.

UBANI-UVUMBA: Zawadi nyingine waliyobeba majusi ilikuwa ubani. Ubani kama manemane tutakayoyaona hapo mbele, hutokana utomvu wa mti wa pekee unaoitwa mbani au manemane. Utomvu ni machozi ya mti unapokatwa. Utomvu huo ukiganda hukusanywa na kuhifadhiwa. Ubani ukiwa umefungwa tu kwenye mfuko au boksi, unafaa kwa kuuangalia tu, na pengine huwezi kuugundua. Ubani unatambulikana pale tu unapounguzwa. Ukitaka kuufaidi ubani, tia penye makaa ya moto, ndipo unaleta harufu nzuri. Ndiyo maana ubani unaitwa pia uvumba, na manemane huitwa manukato.

Tungeweza pia kuita "perfume" – msamiati utokanao na maneno mawili ya kilatini "per fumare" – kwa njia ya moshi. Kutokana na hali yake ya kunukia ubani unatumika katika mazingira mengi sana. Ubani unasafisha hewa ya mahali ilipochafuka kwa namna mbalimbali hata, kwa uhasama, wasiwasi, machungu, magomvi, masikitiko. Harufu ya ubani inamliwaza mtu kiakili. Paolo anasema: “Nimepokea toka mkono wa Epafrodito vitu vile vilivyotoka kwenu, harufu ya manukato, sadaka yenye kibali, impendezayo Mungu” (Fil.4,18)

Harufu ya ubani ni alama pia ya upendo. “Mkaenende katika upendo, kama Kristu naye alivyowapenda ninyi; tena akajitoa kwa ajili yetu, sadaka na dhabihu kwa Mungu kuwa harufu ya manukato” (Ef.5,2). Harufu ya ubani kwa ajili ya tafakari na sala. Katika zaburi sala na masifu kwa Bwana yanalinganishwa na harufu tamu ya ubani ipae juu “Sala yangu ipae mbele zako kama uvumba” (Zaburi 140). Hadi sasa ubani unatumika wakati wa ibada kama alama ya uabudu na ya sala, ya kuheshimu mtu au kitu wakati wa madhehebu. Kwa hiyo moshi wa ubani ni alama ya sala zinazopaa mbinguni na hulinganishwa pia na majitolea ya mashahidi mashemasi Stefano na Laurenti.

Majusi walibeba tunu ya ubani – uvumba, uliokuwa umefungwa katika boksi wakaenda kumfungulia mtoto Yesu. Nadhani uliunguzwa mbele yake, hasa ukizingatia palikuwa na hewa ya kizizini. Sisi wenyewe na imani yetu ni ubani. Lakini endapo imani hiyo inabaki imefungwa tu ndani ya mtu au ndani ya kanisa, imani hiyo inafaa kwa kuiangalia tu, hainukii. Kama ulivyo ubani, imani yafaa iunguzwe ili kueneza harufu ya Kristo.

Kama vile leo iitwavyo Tokeo la Bwana, maana yake Kristu anaonesha utukufu wake unaoshinda giza lililobado limetanda ulimwenguni. Ni jukumu lako mkristu kama hawa majusi, kuonesha au kudhihirisha mpango wa Mungu kwamba watu wameitwa kushiriki urithi huohuo kushiriki mwili huohuo kushiriki katika ahadi hiyohiyo kwa njia ya injili. Yabidi kuifukiza harufu nzuri ya imani uliyo nayo. Je, ni nani hao wanaotakiwa kufukiziwa perfume hiyo ya ubani? Kwanza kabisa Mungu mwenyewe, anayetaka tumtolee maisha yetu na sala zetu kama fukizo kuonesha uabudu wetu. Kadhalika watu wengine walioko kila mahali wanaosubiri mchango wetu wa kushirikisha harufu hii tamu ya Neno la Mungu.

Wanaweza kuwa vijana waliokosa mwelekeo wa maisha, wazee waliosahauliwa, wagonjwa, vilema, watoto, maskini hata maadui wetu nk. Wanaosubiri mchango wetu katika imani, kama vile harufu nzuri ya ubani uliounguzwa na kueneza harufu nzuri ya upendo wa Yesu Kristu. Lakini, yabidi pia kuwa makini unapofukiza ubani wako, kwa wengine wanayo alleji ya moshi. Moshi ambao hata kabla ya kuunusa unaanza kuukohoa na kutoroka. Kumbe ubani wenye moshi mtamu unaonukia na usiokuwa na alleji kwa yeyote yule ni upendo. Ule uwezo wa kujibu mahitaji, matatizo na mategemeo ya watu wa leo. Huo ndiyo ubani unaotegemewa, huko ndiko kuunguzwa, ndiyo ushahidi katika Kristu. Hiyo ndiyo imani ya kweli.

MANEMANE - MANUKATO: Zawadi ya tatu waliyobeba majusi ilikuwa Manemane. Manemane, maana yake “chungu”. Asili na jinsi inavyopatikana manemane ni kama ile ya ubani. Manemane yalijulikana na kutumika katika Misri ya kale katika kupaka maiti. Kadhalika huko mashariki ya mbali manemane yalitumika kumhifadhi marehemu. Katika Biblia, manemane ni moja ya vitu muhimu vinavyochanganywa kwenye mafuta matakatifu (Kutoka 30:23). Manemane yalitumika pia kama dawa, kwa ajili ya kuponya au kupunguza maumivu, yasemwa hata Yesu alipokuwa anateswa alipewa mvinyo uliotiwa manemane lakini hakupokea (Mk. 15:23). John anasema Nikodemu alileta paundi 75 za manemane kumpaka Yesu alipoingizwa kaburini.

Siku za leo manemane yangeweza kulinganishwa na dawa za kuhifadhia maiti. Katika maduka mengi hasa huko ulaya yanauza dhahabu tu wameandika “Compro oro” yaani ninanunua dhahabu. Kwetu uswahilini yako maduka mengi yanayouza ubani-uvumba au udi. Lakini maduka machache yanauza “manemane” yaani mafuta ya kuhifadhia maiti.

Mababa wa kanisa, wametaka tuone katika tunu hii ya manemane picha ya Kristu aliyekabili kishujaa mateso na kifo chake kwa ajili ya kuwapenda watu wote. Kwa hiyo manemane ni alama ya mateso, ya kujihatarisha hasa na hasa inamaanisha msiba. Mtu anayekabili mateso na kifo ipasavyo anaitwa shujaa au askari hodari. Kwa hiyo manemane ni alama ya ushujaa wa imani.

Watu wengi leo hatuna ushujaa isipokuwa tunao ushupavu. Ushupavu wa imani maana yake ni ile hali ya kutetea imani yako hadi kufa lakini bila ya kuijua maana yake. Ushupavu aina hiyo tunauita ushirikina. Ushirikina ni kule kuifuata dini na hasa kuitetea bila kuijua. Huo ni uadui mkubwa na mbaya sana unaoweza kuidhurumu dini yako, afadhali mtu yule anayeichukia dini yake lakini anaijua huyo anasaidia kuisafisha dini yake ili ing’ae. Ushupavu mwingine uliojaa woga sana, ni ule wa kuteseka kishahidi kwa kulowa damu za wengine uliowajerui au kuwaua, badala ya kulowa damu za majeraha yako mwenyewe ya kutetea haki za watu na za kuwapenda wengine.

Ni rahisi sana kuiainisha jamii ya leo inapenda aina gani ya maisha. Leo tunayo jamii iliyotawaliwa na utajiri, mali au dhahabu. Yaani watu wanaopenda maraharaha, viongozi wanaojilundikia mali nk. Jamii namna hiyo inapenda pia kusifiwa, kuabudiwa, kupendwa sana, kushabikiwa, yaani kufukiziwa ubani unaonukia. Jumuia ya leo haipendi kusafishwa, wala kuunguzwa hasahasa mateso na kifo kama manemane. Hakuna ushujaa wa kushuhudia imani yako au taifa lako. Wakristu wa leo tunao woga wa kuonesha ushujaa.

Tunaficha imani yetu. Tuangalie sana tusifanye kama wakuu wa makuhani na waandishi wanaojua kila kitu lakini hawafuati ukweli. Kumbe majusi wa leo daima wanatafuta ukweli. Ukweli ambao Pilato anamwuliza Yesu wakati wa kumhukumu “Ukweli ni kitu gani?”

Ndugu zangu, baada ya msafara huu mgumu na Majusi, tunaona kuwa hii siyo tena Happy-funny, bali ni Epifania ngumu. Basi pamoja na majusi hao tujaribu kufungua tunu zetu, na tumwombe mtoto Yesu azipokee. Hata kama ni tunu dhaifu, lakini tumwombe pamoja na kanisa tukisali “Ee Bwana tunakuomba usiziangalie dhambi zetu, bali angalia imani ya kanisa lako. Utujalie amani na umoja kama yalivyo mapenzi yako. Unayeishi na kutawala daima na milele. Amina”.

Tafakari hii imeandaliwa na Padre Alcuin Nyirenda, OSB.








All the contents on this site are copyrighted ©.