Ninakuleteeni kwa furaha ujumbe wa Neno la Mungu tunaposherehekea sherehe ya Epifania,
Tokeo la Bwana, ambayo huadhimishwa kila terehe 6 Januari katika kipindi cha Noeli.
Ni sherehe ambayo Mfalme Masiha anajitambulisha wazi kwa ulimwengu mzima. Ni kwa njia
ya nyota, Mamajusi wanaweza kufika mahali alipokuwa na wakaweza kumsujudia na kumpatia
zawadi zao.
Kumbe, Yesu
Kristo Masiha ni nyota inayaangaza na kuongoza maisha yetu mpaka mwisho wa nyakati
hadi kufika mbinguni.
Katika somo la kwanza tunaona jambo la ajabu na zuri
likitokea. Nabii Isaya yuko katika ndoto anaona Yerusalemu iliyokuwa imeharibiwa kwa
sababu ya vita na mapigano mbalimbali miaka 800 hivi kabla ya Kristo sasa inakuwa
chanzo cha nuru, na utukufu wa Mungu unaonekana juu yake. Mataifa wakiwakilishwa na
Mamajusi wanaijia nuru hiyo. Nabii Isaya anaimba akisema “inua macho yako Yerusalemu
utazame pande zote za dunia, wote wanakusanyana; wanakujia wewe.”
Ni wimbo
wa sifa kwa Yerusalemu, ni kielelezo cha kuzaliwa Masiha na kwamba atakuwa nuru angavu
kwa ulimwengu na mataifa yote watakusanyika kumsujudia na kumtolea zawadi. Habari
na uaguzi huu tunauona vema katika Injili ambapo tunawaona Mamajusi wakitokea pande
zote za dunia wakiongozana kwa ajili ya kwa ajili ya kumsujudia Bwana aliyezaliwa
na zaidi sana aliye nyota ya mataifa, nyota ya milele.
Katika somo la pili
Mtume Paulo anapowaandikia Waefeso anawaambia juu ya kufunuliwa siri za Mungu kwa
njia ya Mitume. Anasema ni kwa njia ya manabii na Mitume na si wanadamu katika vizazi
vingine Mungu amefunua siri yake. Hata hivyo pamoja na kupewa siri hiyo bado mataifa
mengine wanashiriki pamoja nasi ahadi ya Bwana ya kurithi ufalme wake. Hivi Neno la
Mungu linatualika kutambua kuwa sisi sote tuliobatizwa na kupokea mataji matakatifu
tumeshirikishwa katika ukoo wa kikuhani kwa ajili wokovu wetu na wokovu wa ulimwengu.
Katika
somo la Injili tunapata kuona ujumbe wa Neno la Mungu kwa njia ya Mamajusi, wamefika
kwa mfalme Herode na wanamwuliza yuko wapi mfalme wa Wayahudi? Kwa maana tumeona nyota
yake mashariki nasi tumekuja kumsujudia. Herode anashangaa kwa kufadhaika na anauliza
habari kwa wakuu wa makuhani na waandishi akisema, Kristu azaliwa wapi? Wanamjibu
pasipo kusita, Betlehemu. Anawaagiza Mamajusi wakati wakishamwona Kristo, wamletee
habari ili naye akamsujudie! Mamajusi hawa wanaongozwa na nyota mpaka pale alipo mtoto
na hawatarudi kwa Herode kwa sababu Herode anayo nia ya kutaka kumwua Mwana wa Mungu.
Mamajusi wako katika msingi uleule wa nabii Isaya anaposema Yerusalemu ikiangaza
watu wote watakuja na kumiminika katika mji. Kumbe Mamajusi wanatimiza ule uaguzi
wa nabii Isaya, wanaleta manemane, dhahabu na uvumba. Mamajusi ni kiwakilishi cha
watu wote wanaokubali kuongozwa na ujumbe wa amani, ujumbe wa Yesu Kristo Masiha yaani
nyota, nuru ya ulimwengu. Ni alama ya kanisa lililo jumuiya ya watu wenye chimbuko
moja yaani Mungu mmoja , lakini lugha, tamaduni, umri, kabila tofauti. Watu hawa wote
wako mbele ya nyota angavu ndiye Mkombozi aliyezaliwa.
Mpendwa msikilizaji,
unaalikwa basi leo na Neno la Mungu kujiweka chini ya maongozi ya Nyota angavu, nyota
ya milele ndani ya Kanisa familia ya Mungu. Ninakutakieni heri na baraka za Mungu,ukazidi
kuongozwa na Kristo mwenyewe, daima ukampe hazina stahili kama Mamajusi kwa sifa na
utukufu wa Mungu na pia kwa wokovu wako. Heri na baraka kwa wale walio na majina ya
Epifania na majina ya Mamajusi yaani Gaspar, Melkiori na Barthazari. Mkakomae katika
kusujudu na kumtolea Mungu vipaji vyenu kama kielelezo cha kuongozwa naye katika maisha
yenu. Tumsifu Yesu Kristo.
Tafakari hii imeletwa kwako na Padre Richard Tiganya
C.PP.S.