Baba Mtakatifu Francisko alipokuwa anaadhimisha kumbu kumbu ya miaka 77 tangu alipozaliwa,
aliridhia ombi la Kardinali Angelo Amato la kutaka Pietro Favre atangazwe kuwa mtakatifu
kwa kufuata kanuni mlinganyo! Takwimu zinaonesha
kwamba, ni watakatifu 40 tu ambao wametangazwa kwa kuzingatia sheria hii katika historia
ya Kanisa. Kati yao ni Mtakatifu Gregori VII, Getrude wa Helfta. Petro Damian, Cyril
na Metodi; Yohane wa Damascene, Mwenyeheri Beda, Albert Mkuu, Thomas More na Yohane
wa Avila. Itakumbukwa kwamba, Baba Mtakatifu Francisko, tarehe 9 Oktoba 2013 ametumia
kanuni hii kumtangaza Mwenyeheri Angela wa Foligno, kuwa Mtakatifu. Kardinali Amato
anasema kwamba, ili mwamini aweze kutangazwa kuwa Mtakatifu kwa kuzingatia kanuni
mlinganyo kuna haja ya kuwa na sifa kuu zifuatazo: Ibada kwa mtakatifu husika. Kwa
miaka mingi waamini walimkimbilia Mwejnyeheri Pietro Favre kama mwombezi mwema mbele
ya Mwenyezi Mungu. Watu waliokimbilia msaada wa maombezi yake walijaliwa kupata yale
waliyoomba. Pili, Mwenyeheri anapaswa kuwa na kumbu kumbu za kihistoria zinazoonesha
alama na karama zake za utakatifu, kwa mwenyeheri Pietro Favre, Myesuiti, kuna nyaraka
mbali mbali zinazoonesha karama na utakatifu wake wa maisha. Tatu ni ushuhuda wa miujiza
inayotendeka kwa maombezi ya mwenyeheri Pietro Favre imeendelea kusikika hadi nyakati
hizi. Sifa zote hizi zimemwezesha Baba Mtakatifu Francisko kutumia kanuni ya mlinganyo
kumtangaza Mwenyeheri Pietro Favre kuwa mtakatifu na mwombezi wa Kanisa zima; kwa
kusali kwa ajili ya maombezi yake; kwa kuonesha katika nia ya misa, bila ya kuwa na
hati maalum wala maadhimisho ambayo kwa kawaida yanafanywa na Mama Kanisa. Historia
inaonesha kwamba, Pietro Favre ni kati ya wanafunzi wa mwanzo kabisa wa Mtakatifu
Inyasi wa Loyola. Alipadrishwa tarehe 15 agosti 1534 na kuwa mwanashirika wa kwanza
wa Wayesuiti kuweka nadhiri zake. Akafariki dunia akiwa na umri wa miaka 40 tu. Tangu
wakati huo, watakatifu na watu mashuhuri ndani na nje ya Kanisa waliwataka Wayesuit
kutoa heshima na upendeleo wa pekee kama walivyokuwa wanafanya kwa Mtakatifu Inyasi
wa Loyola, mwanzilishi wao. Alikuwa ni mtu wa mageuzi, aliyeshiriki kikamilifu
katika kufundisha Katekesi; Maandiko Matakatifu na kuhubiri. Alishiriki katika Mtaguso
wa Trenti. Alikuwa mtiifu kwa ajili ya sifa na utukufu wa Mungu kwa kusali, kusoma
na kutafakari; akaonesha fadhila na moyo wa shukrani. Alikuwa ni mnyenyekevu na mtiifu;
akachagua kumwilisha ndani mwake nadhiri ya Ufukara kwa ajili ya Kristo na Kanisa
lake, kiasi cha kudharauliwa na wengi. Alijitoa bila ya kujibakiza katika huduma wala
hakupenda kupoteza wala kuwapotezea wengine muda, kwani kwake hiki kilikuwa ni kipimo
cha uungwana. Mtakatifu Pietro Favre ni mfano na kielelezo cha Upadre; mtawa na
mtu wa sala, mwaliko kwa Makasisi kuwa kweli ni wahudumu wa Neno, Sakramenti na Maisha
ya Watu wa Familia ya Mungu; daima wakijitahidi kuiga mfano wa Yesu Kristo mchungaji
mwema; ili kuendeleza mchakato wa kazi ya: kufundisha, kuongoza na kuwatakatifuza
watu wa Mungu. Wakleri watumie vyema karama na vipaji vyao kwa ajili ya sifa na utukufu
wa Mungu, Kristo na Kanisa. Alitumia vyema milango yake ya fahamu kwa ajili ya
kutekeleza mapenzi ya Mungu; changamoto kwa wakleri kujenga na kuimarisha moyo wa
udugu na urafiki na: waamini walei, watawa, maskini na matajiri. Wawe tayari kujitoa
bila ya kujibakiza kwa ajili ya Mungu, Kanisa na Jirani zao. Mtakatifu Pietro Favre
ni mfano na kielelezo cha mchakato wa majadiliano ya kiekumene yanayofumbatwa katika
maisha ya sala, upatanisho na mshikamano wa kidugu. Wakati wa masomo na majiundo yake
ya Kikasisi alionja Mafundisho ya Kiluteri, lakini akasimama imara katika imani yake.
Ni mtakatifu aliyependa maisha ya Kijumuiya, kwani kwake, Jumuiya ilikuwa si tatizo
la kutafutiwa ufumbuzi, bali Fumbo linalopaswa kukumbatiwa. Ni mtakatifu aliyetegemea
tunza, msaada na maongozi ya Kimungu. Kwa hakika anasema, Kardinali Angelo Amato,
Mtakatifu Pietro Favre ni mfano na kielelezo cha kuigwa katika maisha ya Kipadre na
Kitawa na kwamba, ni “Jembe” la nguvu katika Uinjilishaji Mpya; tayari kujitosa kimasomaso
kwa ajili ya kutangaza Ufalme wa Mungu. Alijiachilia mikononi mwa Roho Mtakatifu ili
aweze kuwa ni chombo cha kuyatakatifuza malimwengu.