Mshikamano wa upendo na Familia ya Mungu Barani Afrika
Baraza la Maaskofu Katoliki Ubelgiji, kila mwaka ifikapo tarehe 5 Januari, linaadhimisha
Siku ya Bara la Afrika, kama kielelezo cha mshikamano na Familia ya Mungu Barani Afrika.
Kwa namna ya pekee, mwaka 2014 unatoa kipaumbele cha kwanza kwa nchi ambazo ziko kwenye
Eneo la Maziwa Makuu: yaani: Rwanda, Burundi na DRC.
Sadaka yote itakayokusanywa
Jumapili tarehe 5 Januari 2014, itapelekwa kusaidia mchakato wa maendeleo endelevu
katika Eneo la Maziwa Makuu na kusimamiwa na Shirika la Misaada la Kanisa Katoliki,
Caritas. Kanisa Katoliki nchini Ubelgiji limetuma Wamissionari wake kutangaza Injili
ya Furaha na Mshikamano kwa Familia ya Mungu Barani Afrika.
Kumbe, mchango
wa hali na mali kutoka kwa waamini na watu wenye mapenzi mema nchini Ubelgiji unapania
kuwatia ari na moyo Wamissionari wanaojitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya Uinjilishaji
Mpya. Juhudi hizi za Baraza la Maaskofu Katoliki Ubelgiji, zilianza kunako Mwaka 2005.
Mwaka 2013, kiasi cha Euro 31,200 zilitumwa Nchini Rwanda kama kielelezo cha mshikamano
wa sala na upendo uliooneshwa na Waamini wa Kanisa Katoliki nchini Ubelgiji.