2014-01-03 09:09:37

Mchakato wa Uinjilishaji, Jimbo kuu la Seoul!


Neno la Mungu ni nguvu inayosukuma kwa kasi kubwa zaidi mchakato wa Uinjilishaji Mpya, katika ulimwengu mamboleo, ambamo watu wanaonekana kumezwa zaidi na malimwengu. Kutokana na ukweli huu, Neno la Mungu halina budi kuwa ni dira na mwongoz wa shughuli na mikakati ya kichungaji katika maisha na utume wa Kanisa. RealAudioMP3

Hii ni sehemu ya barua ya kichungaji iliyoandikwa na Askofu mkuu Andrew Soo-jung wa Jimbo kuu la Seol, Korea ya Kusini kwa ajili ya Mwaka 2014, Mwaka wa Uinjilishaji Mpya Jimbo kuu la Seoul. Waamini wanahamasishwa kujenga na kukuza utamaduni wa kupenda: kusoma, kulitafakari na hatimaye, kulimwilisha Neno la Mungu katika uhalisia wa maisha yao, kama kielelezo cha Imani tendaji.

Waamini wajenge ujasiri wa kutaka kushirikishana na kumegana Injili ya Furaha kwa kuanzia katika: Familia, Jumuiya ndogo ndogo za Kikristo na mahali pa kazi. Waamini wajitahidi kulifahamu kwa kina Neno la Mungu ili liweze kuwa ni dira na mwongozo wa maisha adili na matakatifu.

Askofu mkuu Andrew Soon-jung anasema, imani inapata chimbuko lake katika Neno la Mungu; inakuwa na kukomaa kwa kuboreshwa na Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki na Mafundisho Jamii ya Kanisa, ili kutoa harufu nzuri inayojikita katika matendo ya huruma na mapendo, kama anavyohimiza Baba Mtakatifu Francisko.

Waamini wanaendelea kuhimizwa kuhakikisha kwamba, matunda ya neema na baraka walizojipatia wakati wa Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, yanaendelezwa kwa ari na moyo mkuu zaidi, ili watu waguswe na ushuhuda unaotolewa na waamini sehemu mbali mbali za Jimbo kuu la Seoul. Ndiyo maana, umuhimu wa Neno la Mungu unapewa kipaumbele cha kwanza katika mikakati ya shughuli za kichungaji Jimboni humo.

Waamini wasome na kulitafakari Neno la Mungu. Mapadre katika mahubiri yao, wahakikishe kwamba, Kristo anakuwa ni kiini cha mahubiri yao na wala si vinginevyo. Familia ya Mungu inahamasishwa kujifunga kibwebwe ili kuwatangazia Watu wa MataifaInjili ya Furaha, inayosimikwa katika imani, matumaini na mapendo kwa Mungu na jirani.







All the contents on this site are copyrighted ©.