2014-01-03 14:46:00

Injili ya Kristo inatangazwa kwa njia ya Unyenyekevu, Udugu na Mapendo makuu!


Baba Mtakatifu Francisko, katika Maadhimisho ya Siku kuu ya Jina takatifu la Yesu, Ijumaa tarehe 3 Januari 2014 ameadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwenye Kanisa la Yesu mjini Roma kwa ajili ya kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa neema na baraka zake kwa ajili ya kutangazwa Pietro Favre kuwa Mtakatifu. Katika mahubiri yake, Baba Mtakatifu anawaalika Wayesuit kumwiga Yesu Kristo katika fadhila ya unyenyekevu; kwa kuwaza, kupenda na kutenda kama alivyofanya Yesu mwenyewe kama inavyojidhihirisha kwenye Fumbo la Msalaba.

Baba Mtakatifu anawahamasisha Wayesuit kujitosa kimasomaso kwa kumpatia Yesu na Kanisa lake kipaumbele cha kwanza badala ya kujitafuta wenyewe; kwa kutenda yote kwa ajili ya sifa na utukufu wa Mungu, vinginevyo Shirika linaweza kuyumba na hatimaye, kusambaratika!

Wayesuit wajitahidi kumtafuta Mwenyezi Mungu maadam anapatikana, wakitambua kwamba, kama binadamu wana mapungufu yao, hivyo wanapaswa kujipatanisha na Mungu, ili kuonja upendo na huruma yake. Wapige moyo konde na kutoka kifua mbele kutangaza Injili ya Kristo kwa ari na ujasiri mkuu, kama alivyofanya Mtakatifu Pietro Favre.

Katika maisha yake, alikuwa ni mtu wa kawaida, mwenye utajiri mkubwa wa maisha ya ndani; akafanikiwa kujenga na kuimarisha urafiki na watu wa matabaka yote ya kijamii. Kwa maongozi ya Mtakatifu Inyasi wa Loyola, alijifunza kufanya maamuzi makubwa katika maisha yake. Alikuwa ni mtu mwenye imani thabiti na mwenye mwono mpana zaidi katika maisha na utume wake.

Baba Mtakatifu anawakumbusha Wayesuit kwamba, nguvu ya Kanisa inatokana na uwezo wake kuratibu na kusimamia mambo chini ya maongozi ya Mwenyezi Mungu. Wawe tayari kusikiliza na kuitambua sauti ya Mungu, kwa kusaidiana wao kwa wao kama inavyobainisha Katiba yao ya Shirika na kama alivyofanya Mtakatifu Favre.

Katika mawazo na matendo yake, alitoa kipaumbele cha kwanza kwa Mwenyezi Mungu, akawa tayari kutangaza Habari Njema ya Wokovu kwa ari na moyo mkuu. Injili ya Kristo inatangazwa kwa njia ya unyenyekevu, udugu na mapendo makuu na wala si kwa fitina wala kijicho! Moyo wa binadamu hauna budi kutamani mambo makuu na yale ya maana zaidi; yaani kwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa Kristo, ili kushiriki kikamilifu katika mchakato wa kumtafuta Mungu; tayari kwenda pembezoni mwa Jamii kuwashirikisha wengine huruma na upendo wa Mungu kwa watu wake.

Baba Mtakatifu anasema, Mtakatifu Favre alifanikiwa kuwa ni msafiri, akiwa amesheheni kiu na njaa ya kumtangaza Kristo, changamoto na mwaliko kwa waamini kufanya tafakari ya kina, katika hali ya sala na ukimya, ili kumwomba Mtakatifu Pietro Favre aweze kuwasaidia kupata ari na mwamko kama wake. Licha ya mapungufu yao ya kibinadamu, bado kama Wayesuit wanayo hamu ya kutembea katika mwongozo wa Yesu mwenyewe; wakiendelea kuishi maisha yenye ari kuu: kwa kuwaza na kuishi kama alivyoishi Kristo kwa njia ya kujitosa bila ya kujibakiza kwa ajili ya Kristo na Kanisa lake.







All the contents on this site are copyrighted ©.