Changamoto za maisha ya kifamilia katika ulimwengu mamboleo!
Mama Kanisa anapoendelea kufanya tafakari ya kina kama sehemu ya Maadhimisho ya Sinodi
Maalum ya Maaskofu kwa ajili ya Familia. Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican inapenda
kukushirikisha tafakari ya kina iliyotolewa na Padre Stefano Kaombe, Paroko wa Parokia
ya Mtakatifu Petro, Jimbo kuu la Dar es Salaam katika Maadhimisho ya Sherehe ya Familia
Takatifu ya Yesu, Maria na Yosefu. Kuna mtoto jana alimuuliza mama yake, “Kwa nini
Yesu, ambayae ni Mungu alimkimbia Herode, mwanadamu anayetak kumuua? Ina maana Mungu
anamuogopa mwanadamu?” Swali hili ungeulizwa wewe leo ungejibu nini?
Watu
wengi wanapta shida kuielewa Injili ya leo. Ili tuweze kuielewa, tunatakiwa tuunganishe
tukio la leo na lile la bustanini Eden. Bustanini Eden Mungu aliwaumba Adamu
na Eva, akawa anashuka kwenda kuongea nao kila siku jioni. Siku moja Nyoka akawaambia
Adamu na Eva kuwa Mungu hataki wawe kama YEYE ndio maana amewazuia kula matunda ya
mti wa katikati, wakiyala watakuwa kama Mungu. Adamu na Eva kwa tamaa ya kutaka
kufanan na Mungu, mwenye mamlaka na uwezo usio na kikomo, wakala tunda la mti wa katikati.
Walitaka kujikweza.
Ndivyo leo tulivyo, wanadamu tunataka kujikweza, tufanane
na Mungu. Matokeo yake tunataka kusifiwa, ukienda kwenye sherehe utasikia “itifaki
imezingatiwa”, ni lazima utambue uwepo wa mtu fulani. Kwa kutaka kufanana na Mungu
mwanadamu anajilimbikizia mali, anatafuta mali kwa kila namna hata ikibidi kuwa fisadi.
Kuna wengine matajiri na bado wanakuwa mafisadi, hawaridhiki. Mko huku kanisani! Mnajilimbikizia
mali ili mfanane na Mungu!
Yesu sasa anakuja duniani. Wakati mwandamu
anataka kujikweza afanane na Mungu, Yesu anajinyenyekeza, anajishusha afanane na mwanadamu.
Hivyo anakuja kama mtoto, anayezaliwa na mwanadamu. Tena anazaliwa katika hali ya
umaskini. Kwenye hori laNg’ombe. Niliambiwa kuhusu tukio lililotokea katika Kigango
cha Parokia moja. Walitengeneza Pango la Mtoto Yesu, Katekista akaenda akachukua mavi
ya Ng’ombe akaweka katika lile Pango, kanisa zima likawa linatoa harufu ya mboji.
Waumini wakagoma kusali katika kanisa kwa sababu ya harufu. Ndimo Yesu alimozaliwa,
katika hori la wanyama na harufu ya mboji ilikuwepo. Inapotokea mwanadamu, Herode
anataka kumuua, Yesu bado anajinyenyekeza, anakimbia, hashindani nae, anakuwa mnyenyekevu. Leo
tunaposherehekea sikukuu ya familia takatifu, tuziangalie familia zetu.
Tuanze
na Yosefu: Yosefu Mtii kabisa- anatii maagizo yote ya malaika, haulizai wala hatoi
sababu ya kutotii. Mtu mwingine aliyewahi kupewa maagizo kama Yosefu ni Musa. Alitokewa
na Mungu katika kijiti kinachowaka moto, akaambiwa “Musa nakutuma chukua taifa langu
ulitoe Misri, ulipeleke nchi ya ahadai.” Musa akaanza kuto visingizio, kwa Mungu kwamba
“Waisrael wana mioyo migumu, pia mimi nina kigugumizi, nitaongeaje nao?” Mungu akamwambia
nitakupa mdogo wako awe masaidizi wako, nitakuwa nawe nikifanya miujiza mbalimbali.
Ndipo Musa akakubali, lakini pamoja na hayo yote, tunajua Musa hakufika nchi ya Ahadi.
Yosefu hatoi sababu yoyote, kwamba labda katika safari atafanyaje akipambana na majambazi,
wanyama wakali au atafikia wapi. Anatii na kutekeleza maagizo ya malaika.
Katika
Biblia nzima ukisoma hakuna sehemu Yosefu anapozungumza, yeye anasikiliza na kutii.
Ukimya unatuingiza ndani kabisa ya uwepo wa Mungu. Yosefu anasikia sauti ya Mungu
kutokana na ukimya wake. Ndio maana leo hii watu wengi hawapendi kuwa kimya, maana
wataingia nadani zaidi ya uwepo wa Mungu, watasikia sauti ya Mungu ikiwaagiza waache
vitu fulani na kutenda impendezavyo Mungu, nao hawataki kuacha wanvyoambiwa wache,
hivyo wanaamua kuwa watu wa kelele, ili wasisikie maagizo ya Mungu.
Maria: Anamwamini
Yosefu kuliko hata malaika. Malaika alipoongea naye, alimuuliza, “Itakuwaje jambo
hili na mimi simjui mume?” Mpaka alipoelezwa ndipo alipokubali. Lakini hatuoni popote
Maaria anapomuuliza Yosefu itakuwaje huko tuendako, tunaona anakwenda na Yosefu kule
ambako Yosefu anampeleka. Wanandoa mnatakiwa lenu liwe moja. Umuamini mwenzio. Nawe
baba uwe mlinzi wa familia yako.
Leo katika ndoa zetu, tunaaminiana hivyo?
Letu ni moja kama wanandoa? Leo wewe Yosefu unailinda familia yako? Mnakuwa na muda
wa kuwa pamoja kama wanafamilia?
Watoto wengi siku hizi wanalelewa na televisheni.
Baba na mama hawapo nyumbani wanatafuta pesa. Yale waliyotakiwa wafundishwe na wazazi
sasa wanafundishwa na programu za televisheni. Leo hii unaambiwa kuna kazi mbili uchague
moja, utachagua ipi? Ya kwanza unapata mshahara mnono sana, ila unapata asilimia tano
tu ya muda wa kukaa na familia yako; ya pili, unapata muda wa asilimia hamsini wa
kukaa na familia yako, ila mshahara sio mnono sana, ni kama laki chahce hivi, utachagua
kazi ipi? Kocha wa timu ya taifa ya Ujerumani, baada ya timu yake kuchukua kombe
la dunia, timu nyingi zilimuita zikiwa tayari kumlipa pesa nyingi sana, lakini yeye
alikataa, akasema kuwa kwa miaka miwili aliyoiandaa timu kwa kombe la dunia, hakupata
kabisa muda wa kuwa na familia yake. Alichotaka ilikuwa nchi yake ipate kombe la dunia,
na hili alikuwa ameshalifanikisha, hivyo ulikuwa ni wakati wa yeye kwenda kukaa na
familia yake. Kwa hiyo alikataa ofa zote. Je wewe leo ungechagua nini? Pesa au familia?
Tunapoadhimisha
sherehe ya familia takatifu, tumuombe Mungu leo atubadilishe, familia zetu ziige mfano
wa familia takatifu. Hivyo basi tukae kimya kwa dakika moja tukitafakari hali ilivyo
katika familia zetu.