Viongozi wapya wa Shirika la Masista wa Huruma, Moshi, Tanzania
Shirika la Masista wa Bibi Yetu wa Kilimanjaro, lenye Makao yake makuu Jimbo Katoliki
la Moshi, Tanzania, hivi karibuni limehitimisha mkutano mkuu wa Saba, uliongozwa na
kauli mbiu “Utumishi wa upendo wa Kristo kwa wokovu wa watu”.
Baada ya sala
na tafakari ya kina, wajumbe 44 kutoka ndani na nje ya Tanzania walishiriki katika
uchaguzi mkuu, ili kupata “majembe mapya” yatakayoliongoza Shirika kwa siku za usoni.
Waliochaguliwa ni: Sr. Theresia Buretta kuwa Mama mkuu wa Shirika. Sr. Amandina
Chuwa, Makamu Mama mkuu wa Shirika. Sr. Piala Olomi, Mshauri. Sr. Suplisia Mushi,
Mshauri. Sr. Marsia Kajuna, Mshauri. Sr. Barbara Kimaro, Mshauri pamoja na Sr.
Apia Macha, Mshauri.
Mkutano ulisimamiwa na kuongozwa na Padre Ignatus Kimaro
wa Jimbo Katoliki Moshi. Itakumbukwa kwamba, Shirika la Masista wa Bibi Yetu wa Kilimanjaro,
lilianzishwa kunako Mwaka 1931 likiwa na hadhi ya Shirika la Kijimbo kwa lengo la
kushiriki katika mchakato wa Uinjilishaji wa kina, unaogusa mahitaji ya mtu mzima:
kiroho na kimwili.
Ni Shirika ambalo linashiriki katika ukombozi wa mwanadamu
katika sekta ya elimu, afya na maendeleo endelevu. Bikira Maria, Bibi Yetu wa Kilimanjaro,
ndiye msimamizi wa Shirika na Masista wanapania kufuata nyayo zake katika Uinjilishaji
wa kina, kwa kumhudumia binadamu: kiroho na kimwili.