2014-01-01 08:17:12

Umuhimu wa kukuza majadiliano ya kina kama njia ya kutafuta suluhu ya kinzani na migogoro ya kijamii!


Kanisa Katoliki nchini Mali limeendelea kuwa mstari wa mbele katika kuwahudumia wakimbizi na wahamiaji wanaotafuta hifadhi na usalama wa maisha yao kutokana na vita pamoja na kinzani za kijamii, kisiasa na kidini. Kwa sasa hali inaonekana kuwa shwari kidogo, lakini bado watu wana wasi wasi mkubwa wa usalama wa maisha na mali zao. RealAudioMP3

Ni maneno ya Askofu Laurent Biefuorè Dabirè wa Jimbo Katoliki Dori, nchini Mali, wakati akizungumza na viongozi wa Shirika la Kipapa kwa ajili ya Makanisa hitaji, kufuatia machafuko ya kisiasa yaliyojitokeza hivi karibuni nchini Burkina Faso. Hali ya usalama si shwari sana Kaskazini wa Burkina Faso, kiasi kwamba, Wamissionari kutoka nje ya Burkina Faso wanatekeleza dhamana na maisha yao katika mazingira hatarishi na kwamba, wanaweza kutekwa nyara.

Vita na kinzani za kijamii na kisiasa nchini humo zimepelekea wimbi kubwa la wakimbizi na wahamiaji wanaoyakimbia makazi yao kwa kuhofia usalama wa maisha na mali zao. Zaidi ya wakimbizi 40, 000 wanahudumiwa katika kambi mbili, lakini hali ni ngumu ikizingatiwa kwamba, hili ni eneo ambalo linakabiliwa na ukame wa muda mrefu.

Shirika la Misaada la Kanisa Katoliki, Caritas Mali linaendelea kutoa msaada wa hali na mali kwa wakimbizi na wahamiaji kutoka Burkina Faso. Askofu Laurent Dabirè anasema kwamba, hali ya usalama ni tete nchini Bukrina Faso tangu mwaka 1991, baada ya Seneti kufungwa kutokana ukata, hali ambayo imepelekea demokrasia kuwekwa “rehani”.

Kanisa Katoliki pia limekuwa mstari wa mbele kuendeleza mchakato wa majadiliano ya kidini na waamini wa dini ya Kiislam wanaounda asilimia kubwa ya wananchi wa Burkina Faso. Lengo ni kutaka kudumisha misingi ya haki, amani, upendo na mshikamano wa kidugu, daima waamini wakiwa mstari wa mbele kulinda na kutetea utu na heshima ya binadamu pamoja na uhuru wa kuabudu. Kanisa pia linatoa huduma isiyokuwa na ubaguzi katika sekta ya elimu na afya.

Jitihada za waamini na wafadhili mbali mbali zinalenga kuchangia katika mchakato wa Uinjilishaji Mpya, dhamana inayovaliwa njuga na Mama Kanisa katika mapambazuko ya Millenia ya Tatu ya Ukristo.








All the contents on this site are copyrighted ©.