2014-01-01 15:08:19

Bikira Maria Mama wa Mungu ni chemchemi ya matumaini na furaha ya kweli!


Bwana awabariki na kuwalinda, Bwana awaangazie uso wake na kuwahurumia, Bwana awainulie uso wake na kuwapa amani. Ni maneno ya Baraka kwa mwanzo wa Mwaka Mpya kutoka katika Maandiko Matakatifu.

Ni maneno yaliyosheheni nguvu, ujasiri na matumaini yalisiyo danganya kwani matumaini haya yanapata chimbuko lake kutoka kwa baraka ya Mwenyezi Mungu na matashi mema ambayo Mama Kanisa anapenda kumpatia kila binadamu, kwa kukimbilia tunza na upendo wa Mungu. Matashi haya yanapata utimilifu wake kwa Bikira Maria, Mama wa Mungu. Hali inayoonesha ubora, dhamana katika imani ya Kikristo.

Hii ni sehemu ya mahubiri yaliyotolewa na Baba Mtakatifu Francisko kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican wakati wa Maadhimisho ya Sherehe ya Bikira Maria Mama wa mungu, sanjari na Siku ya 47 ya Kuombea Amani Duniani kwa Mwaka 2014. Mtaguso mkuu wa Efeso ndio uliotamka na kufundisha kwamba, Bikira Maria ni Mama wa Mungu, Theotokos na mwangwi wake ukaonekana mjini Roma kwa ujenzi wa Kanisa kuu la Bikira Maria mkuu. Hapa waamini wanayo nafasi ya kuheshimu Picha ya Bikira Maria Mama wa Mungu. Ni kilio cha waamini waliowataka Mababa wa Kanisa kutamka wazi kwamba, Bikira Maria ni Mama wa Mungu.

Baba Mtakatifu Francisko anasema, Bikira Maria daima amekuwa mioyoni mwa waamini, katika Ibada lakini kwa namna ya pekee katika hija ya imani ambayo ilifanywa na Bikira Maria katika maisha yake na waamini wanajitahidi kuifuatilia. Bikira Maria ni kielelezo makini cha fadhila ya imani, kwani katika maisha yake hapa duniani ametembea katika njia ya maisha na matatizo kama binadamu wengine, lakini daima amekuwa ni hujaji wa imani ambaye Yesu alimkabidhi kuwa ni Mama wa Kanisa pale chini ya Msalaba.

Baba Mtakatifu anasema pale ambapo Yesu aliona imani ya wafuasi wake inatindika kutokana na matatizo na kinzani akawakabidhi kwa Mama yake Bikira Maria, mwamini wa kwanza kuamini, Mama ambaye imani yake haikupungua hata kidogo! Bikira Maria akawa Mama wa wote pale alipomwona Mwanaye wa pekee akiyamimina maisha yake kwa ajili ya ukombozi wa ulimwengu.

Moyo Mtakatifu wa Maria ukafunuliwa wazi, ili utoe hifadhi kwa wema na wabaya, kwa kupenda kama vile Yesu mwenyewe alivyopenda. Kielelezo makini cha ushuhuda wa imani pake kwenye arusi ya Kana ya Galilaya, alipofanikiwa kuwaonesha watu wa mataifa utukufu wa Mungu. Pale Mlimani Kalvari, moto wa imani uliendelea kuwaka katika Ufufuko wa Mwanaye Mpendwa kwa kuwashirikisha wengine, kwa njia hii, Bikira Maria akawa ni chemchemi ya matumaini na furaha ya kweli!

Baba Mtakatifu Francisko anahitimisha mahubiri yake kwa kusema kwamba, Bikira Maria Mama wa Mkombozi anawatangulia waamini ili kuwaimarisha katika imani, wito na utume wa Kanisa. Kwa njia ya mfano wake wa unyenyekevu, utayari katika kutekeleza mapenzi ya Mungu anawawezesha waamini kumwilisha imani yao katika hija ya Injili ya Furaha bila mipaka. Kwa njia hii, utume wa Kanisa utaweza kuzaa matunda yanayokusudiwa, kwani unaratibiwa na na Umama wa Bikira Maria.

Baba Mtakatifu anawaweka chini ya ulinzi na tunza ya Bikira Maria waamini wote katika hija ya imani, matamanio yaliyomo mioyoni mwao bila kusahau mahitaji yao msingi na yale ya ulimwengu katika ujumla wake; hasa kwa wale wenye njaa na kiu ya haki na amani.








All the contents on this site are copyrighted ©.