2013-12-31 12:33:04

Jipatanisheni, ili kujenga misingi ya haki na amani Sudan ya Kusini


Viongozi wa Makanisa nchini Sudan ya Kusini wanawataka viongozi wa Serikali na Kisiasa nchini humo kusitisha mara moja vita na kuanza majadiliano yanayopania kujenga na kudumisha misingi ya haki, amani, upatanisho na maendeleo ya wengi. Wanasiasa waistumie migogoro ya kisiasa ndani ya vyama vyao kuwasababishia wananchi majanga kwa kuendekeza ukabila usiokuwa na tija wala mashiko kwa maendeleo na ustawi wa wananchi wa Sudan ya Kusini.

Viongozi wa Makanisa wanasema, wanasiasa hawana budi kujipatanisha kwanza na kwamba, vita si suluhu ya migogoro ya kisiasa na kwamba, wao kama viongozi wa kidini wanapenda kukazia kwa namna ya pekee upatanisho miongoni mwa wanasiasa na wananchi wa Sudan ya Kusini katika ujumla wao! Upatanisho ni ufunguo wa migogoro na chanzo cha maendeleo ya wengi na kwamba, vita inayoendelea nchini humo itakuwa na madhara makubwa ndani na nje ya Sudan ya Kusini.

Watu wanaendelea kupoteza maisha yao kutokana na vita; baadhi ya vijana wamejiingiza katika vitendo vya uporaji wa mali za watu na uvunjifu wa misingi ya haki na amani na kwamba, watu wengi wanahofia usalama wa maisha yao. Serikali haina budi kuhakikisha kwamba, inadhibiti vitendo vya majeshi ya ulinzi na usalama kwa ajili ya mafao ya wengi. Wananchi, majirani na marafiki wajitafutie hifadhi katika maeneo salama na wapewe ulinzi wa kutosha!

Viongozi wa Makanisa nchini Sudan wanaendelea kuuomba Umoja wa Mataifa na Mashirika ya Misaada Kitaifa na Kimataifa kuendelea kutoa huduma hii msingi kwa wananchi wa Sudan ya Kusini wanaokabiliwa na hali ngumu ya maisha kwa sasa.







All the contents on this site are copyrighted ©.