2013-12-30 09:50:11

Umuhimu wa kuzingatia rasilimali muda!


Mpendwa Mwana familia ya Mungu katika Kanisa la nyumbani, Tumsifu Yesu Kristo! Tukiwa katika masaa ya mwisho kuelekea kufunga mwaka wa 2013 tangu kuzaliwa kwake YEYE aliyetumwa na BABA; sote tunajawa na shauku ya kuuanza mwaka Mpya wa 2014. Na wengi tunasali kumwomba Mungu mkarimu, atujalie kuuanza mwaka mpya salama. RealAudioMP3
Wapendwa Kanisa la nyumbani, Uhai ni zawadi kutoka kwa Muumba wetu. Na muda pia ni zawadi kutoka kwake aliyepo na anayependa tuwepo. Ni Mungu peke yake ndiye anayejua muda wetu wa kuwapo hapa duniani, kwa sababu ni yeye mwenyewe ndiye ametupatia; na ndiyo maana twakiri kwamba; “ndani yake yeye tunaishi, tunajimudu, na kuwa na uhai wetu” [Mdo. 17:28]. Kwetu sisi, tunaupokea UHAI na MUDA kama zawadi. Ni mwito kwa kila mmoja wetu kuitumia zawadi hii kwa shukurani. Zawadi hii, izae matunda, na iwafaidie wengine.
Na mahali pa kwanza kabisa pa kuienzi zawadi ya muda na uhai ni KATIKA KANISA LA NYUMBANI, YAANI KATIKA FAMILIA. Iwapo katika familia kwa bahati mbaya kabisa, watu hawafundishwi kuheshimu na kutunza zawadi ya uhai na muda, daima tutakuwa ni watu wasiojali uhai wa wengine na hivyo kuwasababishia mateso, na sisi wenyewe kujiletea shida na ugumu wa maisha.
Tunapoomba Mungu atujaalie kuuona mwaka mpya, au wengine tunaomba tujaaliwe maisha marefu duniani. Ni jambo zuri sana unaliomba. Swali linakuja; unaomba maisha marefu ili uwe unafanya nini? Ni nini haswa kinakuthibitisha wewe uendelee kuishi maisha marefu? Kuna mafaa yoyote kwako na kwa jamii inayokuzunguka?
Ni swali dogo, lakini ni la muhimu. Endapo sote tunatambua thamani ya uhai na muda, basi tutajitahidi sana kutumia uhai na muda wetu kwa kuwafaidia wengine. Na ukitaka ujifaidie mwenyewe na wale wanaokuzunguka jifunze kutunza uhai, kutumia karama zako na muda vizuri. Muda ni zawadi na zawadi hutumiwa kwa shukurani. Na muda hauji mara mbili.
Mpendwa, zawadi ya mwaka mpya ipo mbele yako. MAISHA NA MIPANGO. Ni dhambi kuishi tu, bila mpango wowote wa maisha. Una mpango gani wa maendeleo ya kimwili au ya kiroho kwa mwaka ujao? Wapendwa, kwa sababu ya kukosa dhamiri ile ya kujali na kuutumia vizuri muda; wengi sana katika maeneo yetu, tumeendekeza utamaduni wa uvivu.
Katika familia kuna uvivu uliyo kithiri. Mashuleni kuna uvivu uliokithiri, halafu watu wanataka wafaulu tu; maofisini huko kuna uvivu uliokithiri, lakini watu wanataka mishahara ya juu na marupurupu. Yaweza kuwa bahati mbaya hata makanisani tukawa na watu wavivu kupita kiasi, wasiojua thamani ya muda. Matokeo ya uvivu huo, ni kukosa ufanisi katika mambo mengi.
Jambo mojawapo ambalo linatupelekea kuwa na maisha magumu kwa viwango mbalimbali, NI KUKOSA MATUMIZI SAHIHI YA MUDA. Tunapokosa ufanisi sasa, wengi TUNAJENGA UTAMADUNI WA KULALAMIKA TU. Katika familia ya wavivu, baba atalalamika maisha magumu, mama naye atalalamika siku nzima maisha magumu, watoto wote watalalamika nao, mwisho hata jiko na viti vitaanza kulalamika, na hakuna siku wanapotafuta muda kuketi na kuona namna gani wajikwamue na ugumu huo.
Ni kulalamika tu, na kuzungukazunguka kutafuta miujiza. Iwapo kila mmoja analalamika SASA NANI MWENYE KUTIMIZA WAJIBU? Wavivu na walalamishi, wanatabia ya kutoridhika na kutoona jema kutoka kwa yeyote. Daima wataona wanaonewa au wanadhulumiwa tu. Kumbe wanajidhulumu wenyewe kwa kuendekeza uvivu na kukosa kuutumia muda kwa shukurani.
Ndugu Mpendwa, kama mwaka huu unaoisha haukutumia kwa shukurani, tuliitumikisha midomo kwa kulalamikalalamika tu; na tukaiadhibu miili yetu kwa kuendekeza uvivu, basi, kwa mwaka ujao, TUFANYE MAPINDUZI YA FIKRA, yatakayotupelekea katika MAPINDUZI YA MAISHA NDANI YA FAMILIA ZETU. Uvivu awe ni adui yetu mkubwa na tumpige vita kwa moyo wote. Mzee wetu alitufundisha, KAZI NI KIPIMO CHA UTU. Na sisi tunaongeza hapo, UVIVU NI KIPIMO CHA USHETANI. Fanya kazi kwa juhudi sahihi na maarifa sahihi ndani ya muda sahihi.
Wapendwa, tuipokee zawadi ya mwaka mpya, na tuwe tayari kutumia muda vizuri kwa faida yetu na ya wengine pia. Tukwepe utamaduni wa uvivu, unaozaa tabia ya kulalamika mpaka midomo inapinda. Tukwepe tabia ya uvivu inayotuletea madeni yasiyolipika. Muda ni mali.
Kutoka Studio za Radio Vatican, kukuletea kipindi hiki ni mimi Padre Pambo Martin Mkorwe OSB.








All the contents on this site are copyrighted ©.