Changamoto za kifamilia katika ulimwengu mamboleo!
“Ondoka, mchukue mtoto na mama yake, mkimbilie Misri, ukae huko hata nikuambie..”
[Mt 2:13 - 15]` Ni juzi tu tumesherehekea Sikukuu ya Krismasi. Bado tuna joto joto
la Sikukuu hii njema na yenye wingi wa baraka. Na wengine hata keki au vijizawadi
vya Krismasi vipo bado katika makabati au majokofu yao.
Dominika ya leo tunavutwa
kujifunza mengi kutoka kwa familia hii takatifu ya Yosefu, Maria na Yesu. Kutoka kwa
Adam na Eva tulirithi mtindo mbaya wa familia isiyoishi pamoja, isiyopanga pamoja,
isiyomsikiliza mwenziye kwa jema litokalo kinywani mwa Mungu. Ilikuwa familia yenye
kutega sikio kwa ya malimwengu, kwa nyoka, kwa marafiki tu. Tulionja ndani ya
familia hii mgawanyiko, lawama, wivu, kudhaniana vibaya na hata kuuana. Adam na Eva
walipokosea, Adam alilaumu moja kwa moja Mungu wake, “..ni huyu mwanamke uliyenipa..”
Na Watoto wao, Kaini na Abeli katika ujana wao na kazi zao hapakuwa na jicho la kujifunza
kutoka kwa mwenziwe bali wivu na hasira hadi kumuua ndugu yake.
Leo katika
Sikukuu ya Familia Takatifu ya Yosefu, Maria na Mtoto Yesu wanatufunza misingi ya
ukaaji pamoja wa familia, kuamua pamoja, kusikiliza sauti ya Mungu kwa pamoja, haidhuru
imesikika kwa sikio la mmoja kwanza katika ndoa. Hakuna ubishi wala mahojiano. Mafunuo
ya Mungu ni kweli hakika. Na hali hii inaalika mmoja kumheshimu mwenziye kwa kile
alichoona au kufunuliwa na Mungu kuwa ni chema. Misingi hiyo inabeba roho ya kupendana,
kuheshimiana, kujaliana, kuchukuliana katika hali zao na kusameheana.
Yosefu
anaambiwa mchukue mtoto na mama yake aende kule anakoambiwa na malaika. Hii ni changamoto
kwa kwake kwa vile Yosefu toka kuzaliwa hajawahi kufika Misri. Lakini kwa Neno la
Mungu anatii. Ni kama Abrahamu mwingine anayenyofolewa katika nchi aliyoizoea ya Uria
na kwenda nchi asiyoijua.
Leo sisi Mungu anatuambia kama Yosefu haya yafuatayo: -
Mchukue mwanao mpeleke shule nzuri apate elimu bora. Hujui fedha ya ada utapata wapi,
shule yenyewe ipo wapi, na je utamudu hadi mtoto afikie darasa la saba au kidato cha
nne ? kwa mzazi wenye kuthubutu wanajua safari hiyo itawalazimu kupunguza kinywaji
au starehe ili mtoto afikie lengo lake. Wazazi wengi wameishia njiani katika hili
kwa kuchanganya maisha na starehe zilizopitiliza. Watoto wangapi wamefukuzwa shule
kutokana na kutokuwa na karo au mahitaji ya shule? Kusomesha, Matibabu ya Watoto na
Mahitaji mengine ya kifamilia ni safari yetu ngumu ya Misri. Ni lazima tuwe na uthubutu
na kujisadaka katika maisha yetu.
- Yosefu anaambiwa mchukue “mtoto na mama
yake”. Hivi ni wangapi katika Krismasi hii, walitoka na wake zao pamoja kwenda kwa
chakula cha pamoja nje mgahawani au kwa ndugu na jamaa wakaribu ? Wengi waliwaacha
wake zao nyumbani kama pazia au stuli sebuleni. Wengi tunaanza kuona aibu kutoka nje
na wake zetu kwa sababu ya muonekano wao, kupungua viwango au kutokana na kuepuka
kuonekana na yule mwingine wa nje tunayemjali.
Yosefu aliondoka na Maria mguu
kwa mguu hadi Misri. Maana yake, sisi katika tukio la kutoka nje ni vyema kuenda na
ubavu wetu kama si kuwabeba hata watoto wetu. Mungu anayeokoa familia anaokoa familia
yote – yaani, baba, mama na mtoto. Na ili sote waonje wokovu wa Mungu mambo madogo
madogo hubeba wokovu na huwa na ni matendo ya kimungu. “..nilikuwa na kiu, msininyweshe..”(Mt
25:42)
- Watoto hujifunza kutoka kwa wazazi kila tufanyacho pindi tunapokuwa
nao pamoja kwa mandali (picnic) au ufukweni mwa bahari au kwenda kutembelea ndugu.
Na mtoto umleavyo ndivyo akuavyo. Na ndio maana somo la Kwanza la Yoshua bin Sira
linamtaka mtoto aleyefunzwa vizuri na mamaye au babaye achukue wajibu wa kuwatunza
wazazi wake “..Mwanangu msaidie baba yako katika uzee wake, wala usipate kumuhuzunisha
siku zote za maisha yake..”(Yoshua Bin sira 3:12). Wazazi tusipolifanya hili mapema,
watoto wengi watashindwa hata kuwazika wazazi wao. Ni watoto wangapi leo wana
nafasi nzuri ya maisha hapa Dar Es Salaam au mikoani – lakini wanashindwa kumpelekea
kibaba cha unga au kilo ya sukari nusu kilo kwa mzazi wake ? Ni wangapi wanaishi
katika nyumba mithili ya makasri ya kifalme Wakati wazazi wanaishi katika kijumba
cha tope na manyasi juu ? Hii ni matokeo ya kutoonja maisha ya upamoja au kujaliana
toka kwa baba na mama. Tukitaka tulilelewe vizuri na Watoto wetu tuliowasomesha kwa
gharama kubwa, tuanze kuonesha upamoja na mama zao na wao wenyewe wakiwa wadogo. Kinyume
chake, tusipoziba ufu tutajenga ukuta.
Tusali kwa ajili ya familia zetu za
nchi yetu ya Tanzania ambazo zinakabiliwa na changamoto ya malezi, baba wa familia
wawe Yosefu mwingine – na mama wa familia wabebe unyenyekevu na isikivu kama wa mama
Bikira Maria. Na matokeo yake ya wazazi wapendanao yawe yale aliyoona mama mmoja kwa
Yesu, “.. heri tumbo lililokuzaa, na maziwa uliyonyonya..”(Lk 11:27)
Jumapili
Njema ! Padre Benno Michael Kikudo. Jimbo kuu la Dar es Salaam.