Sherehe ya Familia Takatifu ya Yesu, Maria na Yosefu
Mpendwa mwana wa Mungu, leo tunasherehekea na kushangilia sherehe ya familia Takatifu.
Masiha amezaliwa ndani ya familia hii. Ndani ya familia hii kuna majukumu ya kutekeleza
ili Mwana wa Mungu akae mahali stahili na kwa namna hiyo atufundisha namna ya kutenda
na kuishi kwenye familia zetu.
Somo la kwanza
toka kitabu cha Hekima ya Yoshua bin Sira linaweka mbele yetu fahari na heri ya kuwaheshimu
wazazi na kuwatunza katika uzee wao. Heri ambazo ziko wazi kadiri ya somo hili ni
kuwa na uzao, na si uzao tu bali kufurahia uzao huo. Kuwa na maisha marefu na uzee
wa kusifika. Kwa kuwatunza wazazi na kuwapa heshima stahili mmoja afanya malipizi
ya dhambi zake. Kwa hakika somo hili lasisitiza na kuweka mkazo juu ya amri ya nne
ya Mungu. Waheshimu baba na mama upate miaka mingi na heri duniani.
Mtakatifu
Paulo anapowaandikia Wakolosai anafafanua namna ya kuishi na kupendana katika familia.
Anaweka wazi fadhila ambazo zajenga maisha ya familia yaani, unyenyekevu, utu wema,
rehema na msamaha kwa kila mwanafamilia. Kilainisho cha fadhila hizi ni UPENDO kifungo
cha ukamilifu. Kama familia na hasa kila mwanafamilia ataweza kuitikia mwaliko huu
wa Mungu, basi familia nzima itakaa katika utulivu na amani ya kweli yaani inayokuza
mshikamano. Mtume Paulo haishii tu kwenye upendo bila kuweka jambo la kutuweka pamoja
yaani kusikia na kusikiliza sauti ya Mungu kwa njia ya Neno la Mungu. Kwa kutafakari
Neno la Mungu tunajiweka tayari siku zote kukaa na Bwana aliye Neno wa Milele, aliye
nuru angavu tuliyoipokea wakati wa siku ya Noeli.
Pamoja na fadhila nyingine,
fadhila ya utii yatufaa kwanza kwa kutii Neno la Mungu na pili kutii mamlaka iliyowekwa
na Kristu katika familia. Baba ni mkuu wa familia yafaa kumtiii na kumheshimu lakini
yeye mwenyewe lazima aige mfano wa Kristu Mchungaji mwema anayewahangaikia kondoo
wake, Yn 10. Ndiyo kusema aoneshe daima fadhila ya upendo kwa mke wake, watoto wake
na watu wote .
Katika injili ya Matayo tunapata mfano wa familia iliyo katika
mahangaiko ya maisha kama sisi. Familia inayolazimika kwenda uhamishoni Misri. Hivi
leo katika ulimwengu watu wanakuwa wakimbii toka nchi zao kwa sababu za kisiasa kuichumi
na mara zote wanapata mateso. Yafaa kuangalia mifumo yetu ya kisiasa na kiuchumi ili
uweza kupunguza na hatimaye kutokomeza uozo huu. Mpendwa msikilizaji Mama Bikira Maria
na Mtakatifu Yosefu wanakimbilia Misri baada ya tangazo kuwa Herode alitaka kuangamiza
Mtoto Yesu katika kundi la watoto wengine.
Jambo hili si geni kwa watawala
kuwaangamiza watoto hivi leo.Tunakumbuka Farao jinsi alivyowaangamiza watoto wote
wa kiume wa Waisraeli kwa kuagiza watupwe katika mto, Kut. 1:15-22 Katika maangamizi
haya Musa atakuwa mtoto wa pekee atakayeponyoka katika mauaji hayo. Ni katika mantiki
hiyo Herode anapoagiza wauwawe watoto wote katika Betlehemu Mtoto Yesu ataponyoka
na kukimbiziwa Misri. Habari hii atapewa Mt Yosefu kwa njia ya Malaika katika ndoto.
Mpendwa
msikilizaji, Musa kadiri ya simulizi katika kitabu cha Kut. 2:15 atakimbia tena kuuwawa
na kisha ataambiwa na Mungu, rudi Misri kwa maana wale wote waliotaka kukuua wamekwishakufa!
Na kwa namna hiyo, Musa atarudi huko, Kut. 4:19-20. Basi mpendwa msikilizaji maneno
anayoambiwa Musa ndiyo tunayoyapata katika Injili, yaani baada ya kufa Herode, ili
litimie neno lililonenwa na Bwana kwa ujumbe wa nabii, akisema “kutoka Misri nalimwita
mwanangu……kwa maana wamekufa walioitafuta roho ya mtoto”.
Mpendwa mwana wa
Mungu, Mwinjili Matayo ataka kutuambia yakuwa Masiha ni Musa mpya, ndiye atakayeongoza
taifa la Israeli si toka Misri, bali toka ulimwengu kwenda mbinguni. Kwa maneno ya
Injili yaani: kutoka Misri nalimwita mwanangu, mwinjili ataka kutuambia kuwa kama
Waisraeli walivyosafiri kwa kuokolewa toka Misri mpaka nchini mwao, ndivyo Mwana wa
Mungu alipenda kushiriki taabu hiyo, anachagua kuingia na kuchukua mwili wa mtu lakini
pasipo kutenda dhambi na kwa njia hiyo kuweza kumkomboa. Kwa kuwa mtu Mwana wa Mungu
atagusa furaha na mahangaiko ya mwanadamu yaliyo sehemu ya maisha yake. Oneni upendo
wa Mungu kujishusha na kuwa mwanadamu wa ajili yako! Badilika basi kidogo angalau
walau!
Mpendwa msikilizaji wa Neno la Mungu, ni jambo gani jingine waweza kujifunza
tokana na familia hii Takatifu? Jifunzeni kukaa pamoja na kujadiliana kama familia
hii walivyofanya ili waweze kukimbia kifo ambacho kilikuwa kinamnyemelea mtoto wao.
Hatari kama hiyo ni jambo la kawaida katika familia lakini je kuna mipango inafanyika
kwa njia ya kuketi pamoja na kutafakari jinsi ya kutatua shida? Kwa upande wangu naona
katika familia nyingi hakuna kukaa pamoja, hakuna majadiliano ya pamoja bali kila
mmoja katika familia kufanya pekepeke! Hili limeua familia nyingi katika mazingira
yetu.
Utemi katika mfumo dume ni hatari kubwa mno katika maisha ya familia
zetu. Hebu basi mpendwa msikilizaji kuweni wa kwanza kuvunjilia mbali mfumo huo, kwanza
kwa njia ya sala na pili kwa njia ya matendo. Nyenzo itakayokusaidia kufikia mabadiliko
ya kweli ni kujiuliza swali hili daima: Hivi Yosefu na Maria waliwezaje kwendana pamoja,
makubaliano yao yalisukumwa na nini? Kwa hakika wao walijikabidhi mikoni mwa Mungu
na wakaweza kuongozwa na Neno la Mungu. Basi tunawaasa na kuwaonya wale watakaofunga
ndoa wakumbuke si lelema bali wajibu na haki msingi katika ndoa vitekelezwe daima
ili kuijenga na kuilinda ndoa mpaka mwisho wa nyakati.
Basi mpendwa mwana wa
Mungu, hawa tuliowasikia katika Injili wakitenda kazi ya Bwana wanakuwa kichocheo
cha wanafamilia kutenda vema katika familia zao daima wakilenga utukufu wa Kristu
uliokwishafunuliwa kwetu na Bwana mwenyewe. Ninakutakieni heri tele wewe uliyemdau
wa familia na hasa unapoweka nguvu yako kukuza tunu bora za familia, ukiangazwa na
Familia Takatifu ya Yesu, Maria na Yosefu. Heri tena kwa jumuiya zote, parokia zote,
mashirika ya kitawa mliojiweka chini ya usimamizi na ulinzi wa Familia Takatifu. Tumsifu
Yesu Kristo Maria na Yosefu.
Tafakari hii inaletwa kwako na Padre Richard
Tiganya, C.PP.S.