2013-12-24 10:56:10

Vita na kinzani za kikabila ni mambo yanayokwamisha maendeleo ya watu!


Viongozi wa kidini kutoka sehemu mbali mbali za dunia wanaendelea kusali kwa ajili ya kuombea: haki, amani na upatanisho wa kitaifa nchini Sudan ya Kusini ambayo kwa sasa inaelekea kutumbukia kwenye vita ya wenyewe kwa wenyewe na hivyo kuzima kabisa ndoto ya uhuru, ustawi na maendeleo ya wananchi wa Sudan ya Kusini.

Hivi karibuni, Kardinali Peter Tukrson, Rais wa Baraza la Kipapa la haki na amani, Askofu mkuu Justin Welby wa Jimbo kuu la Cantebury, na Kiongozi mkuu wa Kanisa la Kiangalikani duniani; Lorna Hood, Mkuu wa Kanisa la Scotland, waliweka sahihi kwenye tamko la pamoja kwa ajili ya kuombea amani Kusini mwa Sudan kwa kuwasihi viongozi wanaohusika kuweka silaha zao chini na hivyo kuanza mchakato wa majadiliano ya kina ili kupata ufumbuzi wa mgogoro huu unaoweza kusababisha maafa makubwa kwa wananchi wa Sudan ya Kusini ambao waliokuwa na matumaini ya kuona haki, amani na maendeleo vikishika kasi.

Noeli ni siku kuu ya kuonesha mshikamano kwa maskini, wanyonge na wote wanaoteseka na kusukimizwa pembezoni mwa Jamii, ili nao pia waweze kuonja haki na amani inayoletwa na Yesu Kristo, Mfalme wa Amani. Viongozi hawa wa kidini wanakumbusha kwa namna ya pekee, ujumbe wa Baba Mtakatifu Francisko unawataka binadamu kutambua kwamba, wao ni ndugu wamoja, walioumbwa kwa sura na mfano wa Mungu; wanapaswa kupendana na kusaidiana kwa dhati.

Vita, kinzani na migogoro ya kikabila haina tena nafasi, bali waamini na watu wote wenye mapenzi mema wanapaswa kujikita katika kutafuta, kudumisha na kuendeleza amani ambayo kimsingi ni zawadi kutoka kwa Mwenyezi Mungu, lakini inamwajibisha binadamu.

Viongozi hawa wa kidini wanawapongeza viongozi wa Makanisa nchini Sudan ya Kusini wanaoendeleza mchakato wa kutafuta suluhu ya mgogoro huu ambao tayari umekwisha sababisha watu kadhaa kupoteza maisha yao na wengine wengi kuyakimbia makazi kwa kuhofia usalama wa maisha yao!







All the contents on this site are copyrighted ©.