Tanzania yapokea msaada wa Pikipiki 44 kutoka China
Waziri mkuu wa Tanzania Mizengo Pinda amepokea pikipiki 44 zikiwa ni msaada kutoka
Ubalozi wa China na Kampuni ya Fu-Tang ya kutoka China. Amekabidhiwa msaada huo Jumanne,
Desemba 24, 2013 mbele ya viongozi wa wilaya ya Mlele katika hafla fupi iliyofanyika
kijiji cha Kibaoni, wilayani Mlele, mkoani Katavi na kushuhudiwa na wakazi wa kijiji
hicho. Akizungumza na viongozi wa wilaya hiyo pamoja na wakazi wa kijiji hicho
kabla ya kukabidhi msaada huo, Balozi wa China hapa nchini, Dk. Lu Youqing alisema
anaamini kupatikana kwa pikipiki hizo kutasaidia kuleta maendeleo ya haraka ya wilaya
hiyo. “Tunataraji matumizi ya pikipiki hizi yatasaidia kuleta maendeleo ya haraka
na hatimaye kuongeza kipato cha wakazi wa wilaya hii,” alisema Balozi Lu ambaye ofisi
yake imekabidhi pikipiki 20. Alisema wakazi wa nchi yake wanafikia bilioni 1.3
na yeye anatamani kuona walau kila raia wa China akinunua walau kilo moja ya chakula
kutoka hapa nchini ili waweze kuongeza soko kwa mazao yanayozalishwa na wakulima wa
Tanzania. Naye Meneja Mkuu wa kiwanda cha kutengeneza pikipiki cha FEKON ambayo
ni kampuni tanzu ya Fu-Tang, Bw. Zheng Bing alisema mara taratibu zitakapokamilika,
wana lengo la kujenga kiwanda cha kutengeneza pikipiki na kompyuta ili kuongeza ajira
kwa Watanzania. Kampuni hiyo ilikabidhi pikipiki 24. Akipokea msaada huo, Waziri
Mkuu alimshukuru Balozi Lu pamoja na kampuni ya Futang kwa msaada huo na kuahidi kuzigawa
ili ziwasaidie watendaji kusimamia kazi na hivyo kuharakisha kuleta maendeleo kwa
wakazi wa wilaya hiyo. Tuna kata 24, kwenye wilaya yetu kwa hiyo kila kata itapewa
pikipiki moja. Hiyo pikipiki siyo ya Katibu Kata binafsi bali ni ya kata, kwa hiyo
Katibu Kata atakuwa ndiyo msimamizi...,” alisema. Waziri Mkuu ambaye yuko kijijini
kwake Kibaoni kwa mapumziko ya mwisho wa mwaka, alisema pikipiki saba zitapelekwa
kwenye vituo vitano vya afya vya Mamba, Usevya, Inyonga, Katumba na Kanoge na zahanati
za Nsimbo na Kasansa. “Pia tutapeleka pikipiki nyingine nane katika shule za sekondari
za Sitalike, Machimboni, Magamba, Nsimbo na Mtapenda. Nyingine ni Utende, Inyonga
na Kasokola,” aliongeza. Mbali na hao, wengine watakaofadika na mgao huo ni watendaji
wa Chama cha Mapinduzi wa wilaya ya Mlele ambao watapatiwa pikipiki moja, jumuiya
za chama katika wilaya hiyo zitapatiwa pikipiki tatu na moja iliyobakia itagawiwa
kwa Chama cha Mapinduzi Mkoa wa Katavi. Waziri Mkuu aliwashukuru Balozi Lu na Bw.
Tang Hulin kwa msaada huo ambao alisema anaamini utasaidia kusukuma maendeleo ya wakazi
wa wilaya hiyo. Kuhusu uzalishaji wa chakula cha kutosha wakazi bilioni 1.3 wa China,
Waziri Mku alisema itabidi Tanzania izalishe magunia milioni 13 ya nafaka ili iweze
kufikisha lengo alilolisema Balozi Lu. Waziri Mkuu Pinda alishapokea msaada wa pikipiki
23 kutoka kwa wafadhili wengine na kugawa pikipiki sita kwa Jeshi la Polisi, pikipiki
13 kwa vikundi vya vijana na zilizobakia nne alizigawa kwa shule za sekondari.