Wanandoa watarajiwa kukutana na Papa Francisko, hapo tarehe 14 Februari 2014, Siku
ya Wapendanao!
Agano la ndoa, ambalo kwa njia yake, mwanaume na mwanamke huunda kati yao jumuiya
ya maisha yote, kwa tabia yake ya asili liko kwa ajili ya mafao yao na kwa ajili ya
kuzaa na kulea watoto. Agano hili kati ya wabatizwa, limeinuliwa na Kristo Bwana kwa
hadhi ya Sakramenti.
Umoja wa ndoa ya mume na mke hauvunjiki kwani kile alichounganisha
Mungu mwanadamu hana ruhusa ya kukitenganisha! Sakramenti ya Ndoa ni ishara ya umoja
wa Kristo na Kanisa lake. Inawapatia wanandoa neema ya kupendana kwa mapendo ambayo
kwayo Kristo amelipenda Kanisa lake. Neema ya Sakramenti ya Ndoa hukamilisha mapendo
ya kibinadamu kati ya mume na mke; huthibitisha umoja usiovunjika na kuwatakasa wanandoa
katika safari ya uzima wa milele!
Ni kwa kutambua umuhimu wa ndoa na familia
pamoja na changamoto zake katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na
teknolojia, Baba Mtakatifu Francisko ameamua kuitisha Sinodi maalum ya Maaskofu itakayofanyika
hapo Oktoba, 2014. Katika mchakato huu, Baba Mtakatifu Francisko, katika Siku kuu
ya Mtakatifu Valentino, hapo tarehe 14 Februari 2014, Siku ya Wapendanao, atakutana
na kuzungumza na wanandoa watarajiwa mjini Vatican majira ya asubuhi.
Baraza
la Kipapa la Familia linasema, walengwa ni wanandoa watarajiwa wanaoendelea kujiandaa
kwa ajili ya kufunga ndoa ndani ya Kanisa. Kwa wale wanaotaka kushiriki tukio hili
la aina yake katika historia ya Kanisa, wanaalikwa kuwasiliana na Idara ya familia
katika Parokia, Majimbo na Mabaraza ya Maaskofu au katika vyama vya kitume kwa ajili
ya ndoa na familia. Kwa watumiaji wa mitandao ya kijamii wanaweza kuwasiliana moja
kwa moja na Baraza la Kipapa kwa ajili ya Familia kwa anuani ifuatayo: events@family.va
Baba
Mtakatifu Francisko mara kadhaa amewataka wanandoa kuendelea kuishi ile furaha ya
ndoa kwa kukazia uaminifu na mapendo, daima wakisaidiana katika mchakato wa utakatifu
wa maisha, huku wakijitahidi kuiga Familia Takatifu ya Yesu, Maria na Yosefu; kwa
kupokea na kukumbatia Injili ya Uhai, kila mtu akijitahidi kujisadakisha kwa ajili
ya mwenzi wake wa ndoa.
Wanandoa watarajiwa wanakumbushwa kwamba, ndoa ya Kikristo
ni Wito Mtakatifu na Sakramenti kama ilivyo kwa wito wa Kipadre na Kitawa. Wanandoa
kwa upendo na uthabiti wa moyo wanaamua kuwa mwili mmoja na roho moja katika safari
ya maisha yao yote, hadi pale kifo kitakapowatenganisha. Sakramenti ya Ndoa inafumbata
zawadi hii inayopata chimbuko lake kutoka kwa Mwenyezi Mungu! Wanandoa wanaalikwa
kusaidiana ili kuweza kukabili "majanga" ya maisha ya ndoa na familia.