2013-12-20 13:40:09

Jengeni urafiki wa dhati na Yesu ili kumtolea ushuhuda katika medani mbali mbali za maisha!


Baba Mtakatifu Francisko Ijumaa, tarehe 20 Desemba 2013 amewashukuru wanachama wa Umoja wa Vijana Wakatoliki Italia waliofika mjini Vatican kumtakia matashi mema ya Noeli na kuwataka daima kuendelea kuwa ni mawe hai, hali wakiwa wameungana na Yesu Kristo, rafiki na mwenza wa maisha!

Baba Mtakatifu amewakumbusha vijana hawa kwamba, Noeli ni Siku kuu inayoonesha ujio wa Mungu kati ya watu wake ili kuwaokoa, kama ilivyotokea mjini Bethlehemu takribani miaka elfu mbili iliyopita. Imani inamwezesha mwamini kumtambua Mwana wa Mungu aliyezaliwa na Bikira Maria kama kielelezo cha upendo wa Mungu kwa binadamu.

Yesu ni sura ya Mungu asiyeonekana; mwenye nguvu lakini anajionesha katika hali ya mtoto mchanga, kielelezo cha ukarimu na upendo wa Mungu kwa kila binadamu. Hii ndiyo sadaka inayofanywa na wazazi na walezi kwa ajili ya watoto wadogo, wagonjwa na maskini.

Vijana hawa wamekumbushwa kwamba, wanapendwa sana na Yesu anayetaka kujenga urafiki wa kudumu pamoja nao, ili hatimaye, waweze kushirikisha furaha ya kukutana na Yesu katika medani mbali mbali za maisha; daima wakiwa mstari wa mbele kuitolea ushuhuda kama Wakristo kweli wasiokuwa na mawaa!

Wawe tayari kuwasaidia wale wanaohitaji msaada wao; bila kuhukumu wala kuwateta jirani zao. Baba Mtakatifu, mwishoni, amewatakia hija njema ya kutembea wakiwa wameungana na Yesu pamoja na Noeli njema kwa Mwaka 2013.







All the contents on this site are copyrighted ©.