Baba Mtakatifu Francisko, Jumatano tarehe 18 Desemba 2013 amefanya mazungumzo na Papa
mstaafu Benedikto XVI, ili kutakiana kheri na matashi mema kwa ajili ya Siku kuu ya
Noeli na Mwaka Mpya wa 2014. Baba Mtakatifu amekumbusha kwamba, Noeli ni Siku kuu
ya imani, matumaini na mapendo yanayoshinda wasi wasi na woga usiokuwa na kifani.
Noeli iwe ni fursa ya kujinyenyekesha na maskini kwa ajili ya kuwaonjesha
maskini matendo makuu ya Mungu; kujifukarisha, ili maskini nao waonje upendo kutoka
kwa jirani zao. Fadhila ya unyenyekevu imwezeshe mwamini kutumikia na kujitoa bila
ya kujibakiza kwa ajili ya Mungu na jirani, hasa wale wanaosukumizwa pembezoni mwa
jamii.
Baba Mtakatifu Francisko anasema, hawa ndio wagonjwa, maskini, wazee,
wapweke na watoto wanaoathirika kwa namna ya pekee katika vita. Baba Mtakatifu Francisko
anatarajiwa tena kuanza Katekesi zake za kila Jumatano, hapo tarehe 8 Januari 2014.