2013-12-18 12:02:55

Noeli iwe ni siku kuu ya imani na matumaini; mapendo na amani pamoja na mshikamano na maskini!


Baba Mtakatifu Francisko katika Katekesi yake, Jumatano, tarehe 18 Desemba 2013, amewakumbusha waamini kwamba, siku hizi za mwisho mwisho za Kipindi cha Majilio ni mwaliko kwa waamini kujiandaa kiroho ili kumpokea Yesu anayezaliwa tena katika maisha yao.

Baba Mtakatifu anasema, Noeli ni Siku kuu ya furaha na matumaini kwa Mwenyezi Mungu ambaye ameamua kuja na kuishi kati ya watu wake kwa njia ya Mwanaye wa Pekee, Yesu, Mungu kweli na Mtu kweli. Mwenyezi Mungu ameonesha upendo na huruma yake kwa binadamu kwa kuwa ni sehemu ya ulimwengu, licha ya kinzani, mateso na umaskini wake. Yesu ni Emmanueli wa kweli, Yaani Mungu pamoja nasi. Hii ndiyo zawadi kubwa inayoletwa na upendo wa Kimungu; upendo unaoponya na kuleta mabadiliko katika mioyo ya watu kwa kuondoa woga na wasi wasi.

Baba Mtakatifu Francisko anawaalika waamini kufanya tafakari ya furaha kuhusu Fumbo la Noeli, ili hatimaye kutambua kwamba, Mungu amejifanya sawa na binadamu na kwamba, binadamu pia anachangamotishwa kujifanya sawa na Mungu: kwa njia ya unyenyekevu na mshikamano na jirani zake, hususan maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii, kwa kuwa makini ili kusikiliza na kuwatimizia shida zao.

Baba Mtakatifu Francisko anawaomba waamini na watu wote wenye mapenzi mema katika Kipindi cha Noeli ya Mwaka huu, kumwomba Bikira Maria Mama wa Yesu na Mama ya Wakristo, kuwasaidia kuiona ile sura ya Yesu Kristo, Mungu aliyefanyika mtu!

Anawaombea ili waweze kuwa ni miali ya mwanga unaong'ara kutoka mjini Bethlehemu, ili kuleta furaha na amani; imani na matumaini kwa watu wote. Mwanga wa Yesu Kristo Mkombozi uenee katika medani mbali mbali za maisha ya waamini na watu wote wenye mapenzi mema, ili watu washuhudie huruma ya Baba wa mbinguni.

Baba Mtakatifu anawaambia waamini wakati wa Maadhimisho ya Siku kuu ya Noeli, kuhakikisha kwamba, wanawakumbuka pia maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii; Watu wanaoendelea kuteseka kutokana na vita na kinzani za Kijamii, lakini kwa namna ya pekee watoto, ili wote hawa waonje uwepo endelevu wa Yesu katika maisha yao







All the contents on this site are copyrighted ©.