2013-12-17 10:57:56

Vita dhidi ya biashara haramu ya binadamu na utumwa mamboleo!


Wakristo nchini Ufilippini wameungana pamoja ili kusimama kidete kulinda na kutetea utu na heshima ya binadamu dhidi ya biashara haramu ya binadamu pamoja na kuonesha mshikamano na wote wanaotendewa na mikasa hii.

Kikundi cha kiekumune kinachodhibiti biashara haramu ya binadamu na utumwa mamboleo kinasema, kitaendelea kupambana kufa na kupona na wote wanaojihusisha na biashara haramu ya binadamu, hadi pale itakapotokemezwa miongoni mwa Jamii.

Hii ni vita ya muda mrefu inayohitaji ujasiri, ari na moyo mkuu ili kufikia lengo. Majanga ya maisha, umaskini na ujinga wa watu ni kati ya mambo yanayotumiwa na baadhi ya watu kuwatumbukiza wanawake, wasichana na watoto katika biashara haramu ya binadamu, ambayo imeenea sana sehemu mbali mbali za dunia na ni kati ya biashara ambazo kwa sasa zinashamiri kwenye soko la kimataifa.

Akizungumzia kuhusu madhara ya biashara haramu ya binadamu pamoja na utumwa mamboleo, Askofu msaidizi Broderick Pabillo wa Jimbo kuu la Manila anasema kwamba, biashara hii ina madhara makubwa, kumbe ni jukumu la watu wote wenye mapenzi mema kushirikiana na kuweka malengo ya pamoja katika mapambano dhidi ya wafanyabiashara haramu ya binadamu na utumwa mamboleo.

Viongozi wa Makanisa hawana budi kushirikiana na vikosi vya ulinzi na usalama ili kuhakikisha kwamba, lengo hili linafanikiwa, kwa kusimama kidete kulinda na kutetea haki msingi za binadamu pamoja na kubainisha mikakati inayoweza kung'oa tatizo hili kuanzia kwenye mizizi.

Mwishoni, wadau wawe ni mipango ya muda mfupi na mrefu katika kuwasaidia waathirika wa biashara haramu ya binadamu na utumwa mamboleo kwa kuwajengea uwezo wa kujitegemea na kuzitegemeza familia zao.







All the contents on this site are copyrighted ©.