2013-12-17 09:11:45

Shikamaneni na kusaidiana, kwani hakuna mtu anayeweza kujitosheleza mwenyewe!


Askofu mkuu Protase Rugambwa, Katibu mwambata na Rais wa Mashirika ya Kimissionari ya Kipapa amewataka watanzania wanapoendelea kuadhimisha Miaka 52 ya Uhuru kukuza na kuimarisha umoja, upendo na mshikamano wa dhati, daima wakiwa mstari wa mbele kutafuta mafao ya wengi. Waendelee kushikamana zaidi katika maisha ya sala na ibada; wawe tayari kujisadakisha kwa ajili ya huduma kwa watanzania wenzao. RealAudioMP3

Askofu mkuu Rugambwa ameyasema hayo Jumapili iliyopita, tarehe 15 Desemba 2013 wakati alipokuwa anazungumza na watanzania mara baada ya Maadhimisho ya Ibada ya Misa Takatifu kwenye Parokia ya Mama yetu wa La Sallete ambayo ni Parokia ya kitume aliyokabidhiwa Kardinali Polycarp Pengo kadiri ya Mapokeo ya Kikardinali. Watanzania wanapokuwa nje ya nchi waoneshe uzalendo kwa nchi na Kanisa lao.

Askofu mkuu Rugambwa amewakumbusha watanzania kwamba, wanategemeana na hakuna mtu yeyote anayeweza kujidai kwamba, anajitosheleza, kumbe anahitaji kuonjeshwa upendo kutoka kwa watanzania wenzake kwa njia ya mshikamano wa dhati.

Amemshukuru Dr. James Msekela, Balozi wa Tanzania nchini Italia pamoja na uongozi mzima wa ubalozi kwa ushirikiano mzuri uliopo kati ya watanzania wanaosoma na kuishi Roma na Ubalozi. Amemwomba Balozi kuendelea kutoa ushauri kwa wanafunzi pale anapoona inafaa kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya watanzania wote.







All the contents on this site are copyrighted ©.