2013-12-17 08:43:01

Mikakati ya kichungaji mara baada ya Maadhimisho ya Mwaka wa Imani nchini Hispania!


Baraza la Maaskofu Katoliki Hispania katika mkutano wake wa Mwaka uliohitimishwa hivi karibuni linasema kwamba, athari za myumbo wa uchumi wa kimataifa zinaendelea kusababisha majanga makubwa katika familia na maisha ya wananchi wengi Hispania. Umoja na mshikamano wa kitaifa uko katika hali tete kutokana na misimamo tenge mintarafu ndoa na familia.
Bado kuna watu wanaendelea kuteseka kutokana na madonda makubwa yaliyoachwa na vitendo vya kigaidi nchini humo. Bado cheche za madhulumu ya kidini dhidi ya Wakristo sehemu mbali mbali za dunia zinaendelea kusikika na kwamba, kuna haja ya kujenga na kudumisha mshikamano wa upendo na wananchi wa Ufilippini walioathirika kutokana na tufani iliyoikumba nchini hiyo na kusababisha maafa makubwa ya maisha ya watu sanjari na uharibu wa miundo mbinu. Kadiri muda unavyozidi kuyoyoma ndivyo watu wanazidi kusahau taabu na mateso ya wananchi wa Ufilippini.
Haya ni kati ya masuala yaliyojadiliwa na Kardinali Antonio Maria Rouco Varela, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Hispania. Anasema, Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, yatakuwa na maana iwapo waamini wataanza kufanyia kazi changamoto za kiimani, kimaadili na utu wema, zilizopelekea Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita kutangaza Maadhimisho ya Mwaka wa Imani. Mmomonyoko wa tunu hizi msingi unawakumba hata viongozi wa Kanisa wanaojikuta wakimezwa na malimwengu.
Kama anavyoendelea kuhimiza Baba Mtakatifu Francisko, kuna haja ya kufanya toba na wongofu wa kichungaji, ili kuleta mabadiliko makubwa katika maisha na utume wa Kanisa mahalia na lile la Kiulimwengu; daima wakijitahidi kusimama kidete kulinda na kutetea haki msingi za binadamu na mafao ya wengi. Familia na Vijana wanapaswa kusaidiwa ili kukabiliana na changamoto hasi katika maisha yao, kwa kujenga na kuimarisha mshikamano wa dhati.
Kardinali Varela anasema kwamba, ndoa na familia zinakabiliana na hali ngumu katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia, kutokana na ubinafsi unaohatarisha tunu msingi za maisha ya ndoa na familia. Hapa anasema kuna haja ya kukazia majiundo makini kwa wanandoa watarajiwa sanjari na kuendeleza malezi ya ndoa na familia kwa njia ya vyama vya kitume. Baba Mtakatifu Francisko ameona changamoto za ndoa na familia ndio maana ameitisha Sinodi maalum ya Maaskofu kwa ajili ya Familia.
Maaskofu waendelee kuwasindikiza vijana wanaotamani kujenga familia kwa njia ya Sakramenti ya Ndoa, kwa kuwasaidia kutambua kwamba, ndoa si mkataba wa mpito, bali wanandoa wanapaswa kupendana, kusaidiana na kutakatifuzana hadi siku ile kifo kitakapowatenganisha.








All the contents on this site are copyrighted ©.