Happy Birth Day Papa Francisko kwa kutimiza Miaka 77 ya kuzaliwa kwako!
Baba Mtakatifu Francisko, tarehe 17 Desemba 2013 anaadhimisha Miaka 77 tangu alipozaliwa.
Itakumbukwa kwamba, Kardinali Jorge Mario Bergoglio alichaguliwa kuwa Khalifa wa Mtakatifu
Petro hapo tarehe 13 Machi 2013. Ni Papa wa 266 kuliongoza Kanisa Katoliki tangu enzi
ya Mtakatifu Petro.
Baba Mtakatifu Francisko kadiri ya mapokeo na mtindo wake
wa maisha ambao unaendelea kuwashangaza wengi, siku yake ya kuzaliwa hupenda kuiadhimisha
akiwa amezungukwa na watoto, ili kumshukuru Mungu kwa Injili ya Uhai, tayari kusonga
mbele kwa imani na matumaini kutangaza Injili ya Furaha kwa Watu wa Mataifa.
Mwishoni
mwa Juma, Baba Mtakatifu alifanya kumbu kumbu ya kuzaliwa kwake kwa kutembelea Zahanati
ya Watoto wadogo ya Mtakatifu Martha iliyoko mjini Vatican. Ilikuwa ni siku kuu ya
kawaida iliyosheheni furaha inayobubujika kutoka katika maisha ya kifamilia. Baba
Mtakatifu Francisko anaendelea kupokea salam na matashi mema kutoka sehemu mbali mbali
za dunia, lakini kubwa zaidi anawaomba waamini na watu wenye mapenzi mema kuendelea
kumwombea katika maisha na utume wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro.
Idhaa
ya Kiswahili ya Radio Vatican inamtakia kheri na baraka katika maisha na utume wake
kwa ajili ya Kanisa na Ulimwengu kwa ujumla, Mungu na mwanadamu wakipewa kipaumbele
cha kwanza katika hali ya unyenyekevu na ujasiri mkuu.