2013-12-14 11:08:34

Jubilee ya Miaka 50 ya Uhuru wa Kenya, iwe ni fursa ya kujenga na kuimarisha haki, umoja, upendo, msamaha na upatanisho!


Maadhimisho ya Jubilee ya Miaka 50 tangu Kenya ilipojipatia uhuru wa bendera ni changamoto na mwaliko kwa wananchi wote wa Kenya kujikita katika mchakato wa ujenzi wa misingi ya: haki, umoja na mshikamano wa kitaifa; upendo, msamaha na upatanisho wa kitaifa.

Ni ujumbe unaotolewa na Baraza la Maaskofu Katoliki Kenya wakati huu wananchi wa Kenya wanapoendelea kumwimbia Mungu utenzi wa sifa na shukrani kwa Jubilee ya miaka 50 tangu walipojipatia uhuru wa bendera.

Padre Vincent Wambugu, Katibu mkuu wa Baraza la Maaskofu Katoliki Kenya anasema kwamba, Kanisa litaendelea kuwa ni sauti ya kinabii, inayowahamasisha wananchi kupendana, kuheshimiana, kusaidiana, kusameheana na kujipatanisha wao kwa wao! Mshikamano na umoja wa kitaifa ni dhamana inayopaswa kufanyiwa kazi na wananchi wote wa Kenya.

Katika mapambano dhidi ya ukoloni, watu walipigania uhuru wakajikuta wanakinzana kwa misingi ya kikabila. Jubilee ya miaka 50 ua Uhuru wa Kenya, iwe ni fursa ya kufanya tafakari ya kina, ili kutambua mapungufu yaliyojitokeza, tayari kufungua ukurasa mpya!

Mzee Nelson Mandela, awe ni mfano wa kuigwa katika kujenga misingi ya ukweli, upatanisho na amani. Kenya sasa inapaswa kujikita katika mikakati na sera za maendeleo endelevu; kwa kuzingatia misingi ya haki, amani, utawala bora, umoja na mshikamano wa kitaifa. Ni wajibu wa viongozi wa Kenya kuhakikisha kwamba, wanajikita katika kukuza na kudumisha tunu msingi za maisha adili, mafao ya wengi, haki na amani.







All the contents on this site are copyrighted ©.