2013-12-14 07:48:24

Imani na changamoto zake nchini Tanzania


Askofu Michael Msonganzila wa Jimbo Katoliki Musoma, hivi karibuni alifunga rasmi Mwaka wa Imani kwa Ibada ya Misa Takatifu iliyofanyika kwenye Kanisa kuu la Bikira Maria Mama wa Mungu, Musoma. Katika mahubiri yake alikazia mambo makuu matano kuhusu imani yaani: Imani inapaswa kuadhimishwa, kuuishi, kuilinda, kuitetea na kuieneza. Askofu Msonganzila katika mahojiano maalum na Radio Vatican anafafanua zaidi vipengele hivi. RealAudioMP3

Itakumbukwa kwamba, Jimbo la Musoma, limeadhimisha Mwaka wa Imani sanjari na Maadhimisho ya Sinodi ya kwanza ya Jimbo Katoliki Musoma na vikao vya Sinodi bado vinaendelea. Kati ya mada zilizojadiliwa kwenye kikao cha mwisho kilichofanyika kuanzia tarehe 9 hadi 13 Desemba 2013 ni: Liturujia, Utamadunisho, miito na changamoto zake. Wawezeshaji walikuwa ni Padre Romuald Kajara na padre Nicholas Segeja.

Ifuatayo ni risala kwa Askofu Msonganzila iliyotolewa na Padre Valence Matungwa, Mkurugenzi Idara ya Uchungaji, Jimbo Katoliki Musoma.

Mhashamu Baba Askofu Michael Msonganzila, waheshimiwa Mapadre, Watawa na Waamini wote Tumsifu Yesu Kristo…. Sinodi Musoma….

Mhashamu Baba Askofu, tumekusanyika katika Kanisa hili Kuu la Jimbo kwa ajili ya kufunga Mwaka wa Imani katika ngazi ya Jimbo. Mwaka wa Imani, katika ngazi ya Ulimwengu, ulifunguliwa tarehe 11 Oktoba 2012 na Baba Mtakatifu Mstaafu Benedikto XVI na kufungwa tarehe 24 Novemba 2013 na Baba Mtakatifu Francisko huko Vatican.
Katika ngazi ya Jimbo, Mwaka wa Imani ulifunguliwa nawe Askofu wetu wa Jimbo tarehe 18 Desemba 2012 hapa hapa katika Kanisa Kuu.

Mhashamu Baba Askofu, Mwaka wa Imani ulilenga kutoa mwaliko kwa ajili ya wongofu mpya wa maisha katika Kristo na kutoa fursa ya kuvumbua na kujifunza misingi ya Imani yetu. Umekuwa ni kipindi cha kuamsha katika kila mwamini hamu ya kukiri Imani kikamilifu, kwa kujiamini na kwa matumaini ikiwa ni pamoja na kutoa msukumo mpya kwa utume wa Kanisa zima ili kuwaongoza watu kutoka katika maisha ya giza la imani na kuwapeleka mahali pa mwanga, uhai na urafiki na Kristo ambaye anatupatia maisha kamili.

Mhashamu Baba Askofu, kwa namna ya pekee, Mwaka wa Imani umetoa mwaliko wa kukuza uhusiano binafsi na Mungu. Mwaliko huu wa pekee unatufahamisha kuwa Imani ambayo ni zawadi ya Mungu kwa Kanisa lake, inahitaji jitihada ya kila mtu binafsi kuielewa, kuiishi, kuilinda, kuikuza na kuieneza. Kwa jinsi hii, Imani inayopokewa kama zawadi, inamwajibisha kila mmoja wetu awe ishara hai ya uwepo wa Kristo Mfufuka pale mahala anapoishi na kufanya kazi.

Ili kutekeleza mwaliko huo, wa kukuza uhusiano binafsi na Mungu, kila mmoja wetu alialikwa kuzingatia mambo manne kama ifuatavyo;


Kila mmoja wetu amealikwa kushiriki kikamilifu katika maadhimisho ya kiliturjia hasa Ekaristi Takatifu. Hiki ndicho kilele ambapo kazi ya Kanisa inaelekea na papo hapo ni chemichemi zimamotoka nguvu zake zote. Ekaristi Takatifu ni Mkate wa Uzima unaolisha roho zetu na kuziimarisha.


Kila mmoja wetu amealikwa kudumisha na kutoa msukumo mpya wa kupokea mara kwa mara Sakramenti ya Upatanisho. Ni katika Sakramenti hii muumini anakutana na Moyo wa Upendo na wa Huruma wa Mungu Baba. Kanisa ni mlango wa huruma ya Mungu, huruma ambayo inatunyanyua kutoka katika dhambi na kututia nguvu mpya ya kuendelea na safari ya kuelekea utimilifu wa Ufalme wa Mungu. Mwaka wa Imani ulimwalika kila mmoja wetu kutambua kuwa Sakramenti ya Upatanisho ni muhimu sana katika kukuza uhusiano binafsi na Mungu.


Kwa jinsi ile ile tunavyoumega mkate unaolisha roho zetu na kuziimarisha, vivyo hivyo ni muhimu kulimega Neno la Mungu na kujishibisha nalo. Mwaka wa Imani umemwalika kila mmoja wetu kuvumbua tena upya hamu ya kujibidisha kwa Neno la Mungu linaloletwa kwetu kiaminifu kwa njia ya Kanisa.


Huu ni mwaliko wa kila mmoja wetu kuijua imani yake. Mtakatifu Anselmo alikiri kuwa Imani yetu ni imani inayoendana na uelewa na ni imani inayotafuta uelewa (fides querens entellectum). Kwa kuzingatia kuwa Mwaka wa Imani ulienda sambamba na kumbukumbu ya Miaka 50 tangu kuitishwa kwa Mtaguso wa Pili wa Vatikano na miaka 20 tangu kutolewa kwa Katekisimu ya Kanisa Katoliki, kila mwamini amealikwa kuyaelewa matini ya Mtaguso huo na ya Katekisimu. Hii ni pamoja na kujifunza na na kuyaelewa mafundisho ya Imani yanayopatikana katika machapisho mengine ya Kanisa.

Mhashamu Baba Askofu, katika Jimbo letu la Musoma tumeadhimisha Mwaka wa Imani katika maadhimisho mawili makubwa ambayo ni Sinodi ya Jimbo na Matembezi ya Sanamu ya Mama Bikira Maria.

Mhashamu Baba Askofu, Sinodi ya Jimbo letu ilizinduliwa nawe tarehe 19 Mei 2013 na itaendelea hadi tarehe 3 Oktoba 2014. Adhimisho hili la Sinodi ni tunda la Mwaka wa Imani. Licha ya kuwa inaadhimishwa katika Mwaka wa Imani, Sinodi yetu inajumuisha malengo yote ya Mwaka wa Imani katika lengo lake na tena inapanga mikakati ya kudumu ya kuielewa, kuiishi, kuikuza na kuieneza Imani yetu katika mazingira yetu. Kwa sababu hii, adhimisho la Sinodi litaendelea kwa mwaka mmoja zaidi hata baada ya kuhitimisha leo Mwaka wa Imani.

Ni matumaini yetu kuwa kwa njia ya adhimisho la Sinodi, Imani itazidi kuamshwa katika wanajimbo wote. Pia tunatumaini kuwa kila mmoja wetu atazidi kuukuza uhusiano wake binafsi na Mungu kwa njia ya ushiriki mkamilifu katika maadhimisho ya Ekaristi, Kitubio, Neno la Mungu na katika kuyajifunza mafundisho ya Imani. Kwa wachungaji, tunatumaini kuwa adhimisho la Sinodi litawaongezea ari ya kichungaji katika kuzidi kuifundhisha na kuieneza Imani.

Mhashamu Baba Askofu, adhimisho la pili katika Mwaka wa Imani lilikuwa ni matembezi ya Sanamu ya Mama Bikira Maria. Kwa kutambua nafasi ya Mama yetu katika safari ya Imani na kwa kuzingatia kuwa Mama huyu ndiye Msimamizi wa Jimbo letu, tulifanya matembezi hayo katika Jimbo zima. Matembezi hayo yalianzia parokiani ya Komuge (21 Aprili 2013) Dominika ya Kuombea Miito na kuhitishwa katika Kanisa Kuu (21 Novemba 2013) siku ya kutolewa Bikira Maria Hekaluni.

Matembezi yalifanyika kama ifuatavyo;

Matembezi haya yamefika katika kila parokia, kila jumuiya na kila kaya ya Wakatoliki. Ni jambo la kutia moyo kwamba hata kaya za wasio wakatoliki ziliomba kupitiwa na Sanamu ya Mama Bikira Maria. Pamoja na maadhimisho hayo katika ngazi ya Jimbo, kila parokia ilikuwa na matukio na maadhimisho mahalia.

Mhashamu Baba Askofu, tunamshukuru Mwenyezi Mungu kwa neema nyingi alizotujalia katika maadhimisho hayo ya Mwaka wa Imani. Tunaomba ajalie ili mwamko wa Imani tulioupata kwa maadhimisho haya uendelee kuwa ndani yetu daima.

Aidha tunawashukuru wote waliopanga na kufanikisha matembezi ya Sanamu ya Mama yetu Bikira Maria katika ngazi ya Jimbo na kusimamia utekelezaji wake mpaka ngazi ya Jumuiya NdogoNdogo. Shukrani za pekee ziwaendee Mapadre, Watawa, viongozi wa Parokia, Jumuiya na Vyama vya Kitume, wahamasishaji, wote ambao kwa majitoleo yao mbalimbali matembezi hayo yamefanikiwa.

Tunaendelea kuomba ushirikiano katika maadhimisho ya Sinodi yanayoendelea ili nayo yaweze kukamilika kadiri ya mipango na matarajio yetu.

Mhashamu Baba Askofu, baada ya maneno hayo, napenda sasa kukualika utuongoze katika Misa hii Takatifu ya Kuhitimisha Mwaka wa Imani Kijimbo








All the contents on this site are copyrighted ©.