2013-12-13 11:58:19

Papa Francisko mtu mashuhuri kwa Mwaka 2013


Baba Mtakatifu Francisko ameteuliwa na Gazeti maarufu la TIME kuwa ni mtu mashuhuri kwa Mwaka 2013. Akizungumzia uteuzi huu, Padre Federico Lombardi, msemaji mkuu wa Vatican anabainisha kwamba, Vatican kwa ujumla hakushangazwa na uteuzi huu, kwani kuna vielelezo makini vinavyoonesha mguso na mashiko tangu Baba Mtakatifu Francisko achaguliwe kuliongoza Kanisa Katoliki kama Khalifa wa Mtakatifu Petro.

Padre Lombardi anasema, hili ni jambo jema kuona kwamba, hata magazeti ya kimataifa yameona na kutambua mchango wa Baba Mtakatifu Francisko, mtu ambaye kimsingi anapenda kujikita katika tunu msingi za maisha ya kiroho, kidini, maadili na utu wema. Baba Mtakatifu Francisko ameendelea kujipambanua kwa kuwa ni sauti ya wanyonge ndani ya Jamii, kiongozi anayetetea misingi ya haki, amani, upendo na mshikamano wa kidugu.

Padre Lombardi anakumbusha kwamba, Papa Francisko si mtu anayependa kujikuza wala kupewa sifa, kwani yote anayotenda ni sehemu ya mchakato wa maisha na dhamana yake ya kutangaza Injili ya Furaha, Upendo bna Huruma ya Mungu kati ya Watu wa Mataifa. Ikiwa kama mambo haya yanaleta mvuto, mashiko na matumaini kwa watu, basi Baba Mtakatifu Francisko anayo sababu ya kuridhika na kumshukuru Mungu. Lakini Baba Mtakatifu Francisko atafurahi zaidi ikiwa kama walau watu wameufahamu ujumbe na nia yake.







All the contents on this site are copyrighted ©.