Jengeni na kudumisha utandawazi wenye mshikamano wa huduma makini kwa wagonjwa!
Mkutano wa ishirini na nane ulioandaliwa na Baraza la Kipapa kwa ajili ya shughuli
za kichungaji kwa wafanyakazi katika sekta ya afya, uliohitimishwa hivi karibuni hapa
mjini Vatican, umetoa changamoto kwa Jumuiya ya Kimataifa kuhakikisha kwamba, huduma
ya afya inajikita katika utandawazi wenye mshikamano, utandawazi unaoguswa na mahangaiko
ya wagonjwa hata wale waliokufani, kwani wao pia wanahitaji kuonja huruma na msaada
kutoka kwa wengine.
Ni huduma
ambayo inapaswa kutolewa kwa kuzingatia kanuni maadili, sheria, utu na maisha ya binadamu.
Itakumbukwa kwamba, mkutano huu, ulikuwa unaongozwa na kauli mbiu “Kanisa
katika huduma kwa wazee wagonjwa: tiba kwa wagonjwa wenye matatizo ya mishipa ya fahamu”
Askofu mkuu Zygmunt Zimowski, Rais wa Baraza la Kipapa kwa ajili ya shughuli za kichungaji
kwa wafanyakazi katika sekta ya afya anabainisha kwamba, mkutano huu umehudhuriwa
na idadi kubwa ya wajumbe wapatao 700 kutoka katika nchi 57.
Ni watu waliotoka
katika medani mbali mbali za maisha ya mwanadamu: kiuchumi, kisiasa na kitamaduni.
Wameshirikishana, ujuzi, mang’amuzi, wasi wasi na vipaumbele vyao kwa ajili ya huduma
kwa wagonjwa mahali popote pale walipo. Ni mkutano ambao umewashirikisha pia wajumbe
waliokuwa na imani na dini tofauti, lakini wote kwa pamoja wamemwangalia mgonjwa,
aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu.
Mkutano huu umekuwa ni jukwaa la majadiliano
ya kina, kama ambavyo anaendelea kukazia Baba Mtakatifu Francisko kama sehemu ya mchakato
wa kuwatangazia watu Injili ya Furaja, ili kuweza kukua na kukomaa kwa kuwasikiliza
wengine. Utu na heshima ya binadamu hata pale wanaokuwa wanateseka na kushambuliwa
na magonjwa, bado wanapaswa kuheshimiwa na kuthaminiwa.
Wajumbe wamepinga
kwa kauli moja utamaduni wa kifo na badala yake, wanaendelea kuhimiza waamini na watu
wenye mapenzi mema kujikita zaidi katika kutangaza Injili ya Uhai, dhidi ya sera zinazokumbatia
utamaduni wa kifo. Wajumbe wamekubaliana kimsingi kwamba, hata pale sera za kifo laini
zinapotangazwa na kuonekana kana kwamba, ni huruma kwa wagonjwa, lakini hapa kinachopewa
msukumo zaidi ni masuala ya uchumi na wala si utu na heshima ya binadamu aliyeumbwa
kwa sura na mfano wa Mungu. Haya ni machozi ya mamba! Hapendwi mtu, ila pochi ndiyo
inayotafutwa kama wanavyosema Waswahili wa Pwani!
Gharama za tiba zinaendelea
kupanda siku hadi siku kutokana na kuongezeka kwa umri wa watu kuishi na waathirika
wakubwa ni wazee. Shirika la Afya Duniani, WHO linasema, kuna haja ya kuwa na mikakati
makini ya huduma za afya kwa waathirika wa magonjwa ya mishipa ya fahamu. Kwa sasa
wagonjwa hawa wamefikia millioni 35. Inakadiriwa kwamba, ifikapo mwaka 2050 wagonjwa
hawa watakuwa wamefikia millioni 100.
Kumbe, kuna haja ya kujenga utamaduni
wa mshikamano katika utandawazi unaoguswa na mahangaiko ya watu, ili kuwajengea matumaini
ya kuweza kupona. Ni mshikamano unaopaswa kufanywa na wadau mbali mbali katika sekta
ya afya na Kanisa lina uwezo mkubwa wa kuhamasisha jambo hili. Magonjwa mengi yanayotokana
na uzee yanaweza kupatia tiba kwenye nchi zilizoendelea, lakini jambo la msingi ni
kuhakikisha kwamba: kanuni, maadili, utu na heshima na maisha yabinadamu yanapewa
kipaumbele cha kwanza.
Askofu mkuu Zymunt Zimowski anasema, utandawazi wa
huduma ya afya unaojali, ni jambo linalowezekana, kwa ajili ya wagonjwa wenye kuhitaji
tiba na huduma, ikiwa kama watu watatekeleza wajibu na dhamana ya kulinda na kutetea
Injili ya Uhai.