2013-12-13 07:27:15

Bado Wakristo wanaendelea kudhulumiwa hata katika nchi zile zinazodhani kuwa zina demokrasia ya kweli!


Askofu mkuu Dominique Mamberti, Katibu mkuu wa mambo ya nchi za nje na ushirikiano wa kimataifa mjini Vatican, hivi karibuni ameshiriki katika mkutano wa ishirini wa Mawaziri wa ulinzi na usalama na ushirikiano wa kimataifa kutoka katika nchi za Ulaya, OSCE, uliokuwa unafanyika mjini Kiev, Ukraine kwa kusema kwamba, Wakristo wanadhulumiwa na kunyanyaswa hata kwenye nchi zile ambazo zina demokrasia. RealAudioMP3

OSCE katika kipindi cha miaka kumi iliyopita imejitahidi kutekeleza wajibu wake kikamilifu hasa katika masuala ya udhibiti wa silaha na sera za kijeshi. Ujumbe wa Vatican umeonesha kutoridhika kwake kutokana na kusuasua kwa utekelezaji wa Hati ya Vienna, inayokazia ukweli na uwazi kuhusu masuala ya kijeshi sanjari na amani na utulivu kwa nchi wanachama.

Askofu mkuu Mamberti, akizungumzia kuhusu uchumi na mwelekeo wake katika utunzaji bora wa mazingira, amezitaka nchi wanachama kuonesha utashi wa kisiasa katika mchakato unaopania kulinda na kutunza mazingira, sanjari na matumizi bora ya nishati rafiki kwa ajili ya maendeleo ya wengi.

Wajumbe wa OSCE wamejadili pia kuhusu tatizo la wakimbizi na wahamiaji Barani Ulaya. Ujumbe wa Vatican kwenye mkutano huu umekazia umuhimu wa kulinda na kudumisha haki msingi za wakimbizi na wahamiaji, hata wakati huu nchi nyingi za Ulaya zinapokabiliana na athari za myumbo wa uchumi kimataifa. Wahamiaji wasiangaliwe tu kama nguvu kazi ya mpito, bali raia wenye utu, haki na wajibu wa kutekeleza katika jamii inayowpatia hifadhi.

Askofu mkuu Mamberti anasema, biashara haramu ya binadamu ni jambo ambalo linaendelea kuongezeka kwa kasi kubwa duniani, kumbe, kuna haja kwa Jumuiya ya Kimataifa kulivalia njuga tatizo hili linalodhalilisha utu na heshima ya binadamu. Mwelekeo na mwono sahihi wa binadamu; uhuru wa dhamiri na wa kidini ni kati ya mambo nyeti yaliyojadiliwa na wajumbe wa mkutano wa OSCE. Inasikitisha kuona kwamba, hata baada ya karne kumi na saba za uhuru wa kidini Barani Ulaya, kuna baadhi ya mataifa ambayo yanaendeleza dhuluma na nyanyaso za kidini dhidi ya Wakristo.








All the contents on this site are copyrighted ©.