Abiria 12 wafariki dunia na wengine 71 wajeruhiwa kutokana na ajali ya Bus, Tanga
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Mrisho Kikwete amemtumia Salamu za
Rambirambi Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Lt(Mst) Chiku Galawa kufuatia vifo vya watu 12 na
wengine 71 kujeruhiwa baada ya basi Na. T610 ATR la Kampuni ya Burudani lililokuwa
likitokea Korogwe kwenda Dar es Salaam kupinduka katika Kijiji cha Taula mapema asubuhi
ya tarehe 12 Desemba, 2013.
“Nimepokea kwa mshtuko na masikitiko makubwa taarifa
za vifo vya watu 12 vilivyotokea tarehe 12 Desemba, 2013 huku wengine 71 wakijeruhiwa,
baada ya basi la Kampuni ya Burudani walilokuwa wakisafiria kutoka Korogwe kuelekea
Dar es Salaam kupinduka katika Kijiji cha Taula”, amesema Rais Kikwete katika Salamu
zake.
Rais Kikwete amesema vifo vya watu hao ni pigo kubwa siyo tu kwa familia
za watu waliopoteza ndugu zao katika ajali hiyo, bali pia Taifa letu kwa ujumla ambalo
limepoteza nguvu kazi muhimu iliyokuwa bado inahitajika kwa ujenzi wa Taifa.
“Kutokana
na msiba huo mkubwa uliotokea katika eneo la Mkoa wako, ninakutumia Salamu za Rambirambi
kutoka dhati ya moyo wangu wewe Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Mheshimiwa Lt. (Mst) Chiku
Galawa kwa kupoteza watu wengi kwa mara moja katika ajali hiyo. Namuomba Mwenyezi
Mungu, Mwingi wa Rehema azipokee na kuzilaza Mahala Pema Peponi Roho za Marehemu wote,
Amina”.
Rais Kikwete amemuomba Mkuu wa Mkoa wa Tanga kumfikishia Salamu zake
za Rambirambi na pole nyingi kwa familia, ndugu na jamaa waliopotelewa na wapendwa
wao katika ajali hiyo, lakini amewahakikishia kwamba yuko pamoja nao katika kipindi
hiki cha maombolezo. Amewaomba wawe na moyo wa uvumilivu, ujasiri na subira katika
kipindi hiki kigumu wanachopitia wakiomboleza vifo vya ndugu zao.
Aidha Rais
Kikwete amesema anawaombea kwa Mwenyezi Mungu majeruhi wote wa ajali hiyo waweze kupona
haraka na kurejea katika hali zao za kawaida, ili waungane tena na ndugu na jamaa
zao na kuendelea na maisha yao kama ilivyokuwa kabla ya kutokea kwa ajali.