2013-12-12 08:30:43

Maandalizi ya Siku ya Vijana Duniani kwa Mwaka 2016 yaanza kutimua vumbi!


Kardinali Stanislaw Dziwisz, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Krakovia, Poland, hivi karibuni ametangaza kwamba, kuanzia tarehe 25 Julai hadi tarehe Mosi Agosti 2016, Jimbo kuu la Krakovia, litakuwa linaadhimisha Siku ya 31 ya Vijana Duniani inayoongozwa na kauli mbiu “Heri wenye rehema maana hao watakuwa na rehema. Mt. 5:7. RealAudioMP3

Maadhimisho haya ni uamuzi uliotolewa na Baba Mtakatifu Francisko mara baada ya Maadhimisho ya Siku ya 28 ya Vijana Duniani kwa Mwaka 2013 yaliyofanyika mjini Rio de Janeiro, nchini Brazil.

Vijana kutoka kona mbali mbali za dunia, watafika na kushuhudia mahali alipozaliwa, akaishi na kulitumikia Kanisa kama Padre, Askofu na hadi pale alipochaguliwa kuwa Khalifa wa Mtakatifu Petro. Hili ni tukio la kimataifa litakalokuwa ni mwendelezo wa Maadhimisho ya sherehe na shamra shamra baada ya Mama Kanisa kumtangaza Mwenyeheri Yohane Paulo II kuwa Mtakatifu hapo tarehe 27 Aprili 2014.

Vijana wengi wameonesha nia na hamu ya kushiriki kwa mara nyingine tena katika tukio hili la kiimani ambalo limekuwa ni la pekee katika maisha na utume wa Mama Kanisa kwa vijana. Tayari Jimbo kuu la Krakovia limekwisha anzisha tovuti inayoendelea kusimulia maandalizi ya Maadhimisho ya Siku ya 31 ya Vijana Duniani kwa Mwaka 2016.

Baba Mtakatifu Francisko tayari amekwisha toa kauli mbiu ya Maadhimisho ya Vijana Kijimbo la Kimataifa kuanzia mwaka 2014 hadi Mwaka 2016. Kwa wale wanaopenda kujihabarisha zaidi wanaweza kufuatilia habari hizi kwenye mtandao wa Jimbo kuu la Krakovia kwa ajili ya Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani kwa Mwaka 2016 kwa anuani ifuatayo: krakow2016.com

Kama kawa! Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican kwa njia ya mtandao wake itaendelea kukujuza yale yanayojiri kuhusiana na maandalizi haya; ukiona inapendeza mshirikishe jirani yako pia, kwani mambo mazuri ni kushirikishana!








All the contents on this site are copyrighted ©.