2013-12-11 13:53:17

Tata Madiba atakumbukwa na wengi!


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Mrisho Kikwete, Jumanne, Desemba 10, 2013, ameungana na viongozi wa mataifa mbali mbali duniani na maelfu ya wananchi wa Afrika Kusini Kuadhimisha Kumbukumbu ya Kifo cha aliyekuwa kiongozi mashuhuri wa Afrika Kusini na duniani, Marehemu Nelson R Mandela.

Maelfu kwa maelfu ya wananchi wamehimili mvua kubwa iliyokuwa inanyesha kwa nguvu kwenye Uwanja wa Michezo wa FNB mjini Johannesburg kumwaga Mzee Mandela ambaye alikuwa ishara kuu ya upinzani wa siasa za ubaguzi wa rangi za makaburu wa Afrika Kusini.

Mheshimiwa Mandela ambaye alifariki dunia Desemba 5, 2013, alikuwa Kamanda wa Jeshi la Ukombozi la Chama cha African National Congress la Umkhoto we Sizwe akafungwa jela kwa uhaini kwa miaka 27 na utawala wa Makaburu.

Baada ya kutoka jela Februari 1990, Mzee Mandela alichaguliwa kuwa Rais wa Kwanza wa Afrika Kusini ya mwaka 1994. Lakini Mheshimiwa Mandela alitumikia kipindi kimoja tu cha miaka mitano na kukataa kutumikia kipindi cha pili.

Kiasi cha viongozi 91 kutoka sehemu duniani wamehudhuria Kumbukumbu hiyo iliyokuwa na kila aina ya mchanganyiko wa hisia – wengine wakiwa na majonzi na wengine wakicheza na kuimba kwa muda wote wa shughuli hiyo iliyochukua kiasi cha jumla ya saa tano.

Mbali na Rais Kikwete ambaye amefuatana na Mama Salma Kikwete, marais wengine mashuhuri duniani waliohudhuria Kumbukumbu hiyo ni Mheshimiwa Barack Obama wa Marekani, Mheshimiwa Francois Hollande wa Ufaransa, Waziri Mkuu wa Uingereza, Mheshimiwa David Cameroun na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa (UN) Ban Ki Moon.

Kumbukumbu hiyo pia ilihudhuriwa na viongozi wa zamani wa Marekani wakiwemo marais watatu wa zamani wa Marekani – Mheshimiwa Jimmy Carter, Mheshimiwa Bill Clinton na Mheshimiwa George W. Bush na mawaziri wakuu wawili wa zamani wa Uingereza, Mheshimiwa Tony Blair na Mheshimiwa Gordon Brown.

Rais Kikwete Jumatano, Desemba 11, 2013, ataungana na viongozi wenzake katika kutoa heshima za mwisho na kuuaga rasmi mwili wa Marehemu Mandela ambao utawekwa kwenye Majengo ya Urais wa Afrika Kusini ya Union Buildings mjini Pretoria.








All the contents on this site are copyrighted ©.