2013-12-11 08:38:34

Tata Madiba, kwa heri! Umekuwa ni daraja la upatanisho kati ya watu wa mataifa!


Mwili wa Marehemu Nelson Mandela, Siku ya Jumatano tarehe 11 Desemba 2013 umewasili mjini Pretoria ambako utakaa kwa muda wa siku tatu, ili kutoa nafasi kwa wananchi wa Afrika ya Kusini kutoka heshima zao za mwisho. Magari ya Polisi yaliusindikiza Mwili wa Tata Madiba kutoka kwenye Hospitali ya Kijeshi.

Maelfu ya watu yalijipanga barabarani kumpungia mkono Tata Madiba anapoelekea kwenye nyumba yake ya mwisho hapa duniani, huko Qunu, Kijijini kwake na hatimaye, kukamilisha hija ya maisha yake hapa duniani, Jumapili tarehe 15 Desemba 2013.

Kati ya matukio makubwa yatakayokumbukwa na Jumuiya ya Kimataifa wakati viongozi wakuu wa Jumuiya ya Kimataifa walipoungana na wananchi wa Afrika ya Kusini kutoka heshima zao za mwisho kwa Mzee Nelson Mandela, mtu wa watu ni kitendo cha Rais Barack Obama wa Marekani kuonana uso kwa uso na hatimaye kushikana mkono na Rais Raul Castro wa Cuba, kitendo ambacho hakijawahi kutokea baina ya wakuu wa nchi hizi mbili, takribani miaka 50 iliyopita. Ndiyo maana Tata Madiba anakumbukwa na wengi kama daraja la upatanisho kati ya maadui, changamoto ya kuendeleza hazina hii kubwa kati ya watu wa mataifa.

Tarehe 10 Desemba 2013, ilikuwa siku muhimu sana kwa wananchi wa Afrika ya Kusini, siku ambayo: umati wa watu kutoka sehemu mbali mbali za dunia, umesimama kuomboleza kifo cha Tata Madiba. Marais, mawaziri wakuu, Maspika wa mabunge na raia wa kawaida, walifika kwenye Uwanja wa michezo ulioko Johannesburg, ili kutoa heshima zao za mwisho. Baadhi ya viongozi hawa wameshangiliwa na wengine kuzomewa! Kardinali Peter Turkson, Rais wa Baraza la Kipapa la haki na amani, alikuwepo jukwaani kumwakilisha Baba Mtakatifu Francisko katika tukio hili la kihistoria.

Ilikuwa ni kumbu kumbu ya Miaka 20 tangu Mzee Nelson Mandela na Bwana F.W. de Klerk, walipotunukiwa tuzo ya amani, kwa Jumuiya ya Kimataifa kutambua jitihada zao za pamoja katika kusitisha utawala wa ubaguzi wa rangi. Viongozi ambao baadaye, walijenga na kuimarisha urafiki wa dhati kati yao! Bwana Klerk, alikuwepo pia uwanjani, kutoa heshima zake za mwisho kwa Tata Madiba!

Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa, Bwana Ban Ki-Moon, ameusifu mchango wa Mzee Nelson Mandela katika mchakato wa upatanisho wa kitaifa. Hakumchukia mtu, bali alichukia chuki na uhasama kati ya watu, akaonesha nguvu ya kusamehe na kusahau. Mzee Madiba ameiachia Jumuiya ya Kimataifa urithi mkubwa ambao ni kama mti mkubwa uliozamisha mizizi yake katika fikira na mioyo ya watu.

Rais raul Castro amegusia uhusiano wa kirafiki uliokuwepo kati ya Mzee Nelson Mandela na Rais Fidel Castro wa Cuba; watu waliosimama kidete kulinda na kutetea utu na heshima ya binadamu; haki, uhuru na demokrasia ya kweli. Mzee Madiba atakumbukwa na wengi kwa kuwa ni "Nabii wa Umoja wa kitaifa, upatanisho na haki".

Rais Barack Obama wa Marekani aliyekuwa anashangiliwa na wengi kutokana na ushuhuda wake kuhusu maisha na changamoto alizopata kutokana na kumfahamu Mzee Nelson Mandela, anasema, Tata Madiba ni kati ya wanasiasa mashuhuri wa Karne ya ishirini na moja, aliyediriki kuwashirikisha wengine wasi wasi, mahangaiko yake ya ndani, mahesabu yake tenge na ushindi mkubwa aliofanikiwa kujipatia wakati wa maisha yake hapa duniani.

Mzee Madiba amekuwa ni sauti ya wanyonge; mtu aliyekazia tunu msingi za maisha ya kimaadili, haki na amani. Itakuwa ni vigumu kwa dunia kumpata Mandela mwingine. Rais Obama amewataka vijana wa Afrika ya Kusini na vijana wengine wote popote pale walipo, kuhakikisha kwamba, wanajitahidi kujichotea hazina kubwa iliyoachwa na Mzee Nelsona Mandela.

Rais Jacob Zuma amemwelezea Mzee Madiba kuwa ni kiongozi jasiri aliyejitosa kimasomaso kwa ajili kulinda na kutetea uhuru wa wote. Ni kiongozi ambaye maisha yake yameacha chapa ya kudumu katika watu wa Mataifa. Serikali ya Afrika ya Kusini itaendelea kuenzi mchango mkubwa wa Tata Madiba katika maisha na ustawi wa wananchi wa Afrika ya Kusini kwa kukazia: demokrasia, utu na heshima ya binadamu; kuendeleza mchakato wa mapambano dhidi ya umaskini, baa la njaa, ujinga, maradhi na ukosefu wa fursa za ajira.

Mwakilishi wa Familia ya Mzee Mandela. Jenerali Thanduxolo Mandela amesema kwamba, wanatambua kwamba, Mzee Madiba alikuwa ni mtu wa watu si tu kwa ajili ya Familia yake, Afrika ya Kusini, bali ni mtu aliyejitoa kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Afrika na Ulimwengu katika ujumla wake.

Askofu mkuu mstaafu Desmond Tutu, amewataka viongozi na wananchi wa Afrika ya kusini kuwa na nidhamu kama njia ya kumuenzi Mzee Nelson Mandela, aliyefariki dunia akiwa na umri wa miaka 95; maisha ambayo ameyasadakisha kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya wananchi wa Afrika ya Kusini.

Viongozi wengine waliobahatika kuhutubia ni pamoja na Rais Dilma Rousseff kutoka Brazil, Bwana Li Yuanchao, Makamu wa Rais wa China, Bwana Hifikepunye Pohamba, Rais wa Namibia pamoja na Bwana Pranab Mukherjee, Rais wa India.







All the contents on this site are copyrighted ©.