2013-12-11 11:18:42

Rushwa ni Janga la Kimataifa


Rushwa ni adui wa haki na ina madhara makubwa sana katika uchumi wa dunia. Inakadiriwa kwamba, rushwa inayotembea na kutembezwa duniani ni sawa na asilimia 10% ya Pato Ghafi la Dunia. Hizi ni takwimu zilizotolewa na Umoja wa Mataifa katika Maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya kupambana na rushwa ya kijamii, kisiasa na kiuchumi iliyofanyika hapo tarehe 9 Desemba 2013.

Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Bwana Ban Ki-Moon katika ujumbe wake kwa maadhimisho haya anasema "rushwa ni janga la kimataifa" inayojionesha si tu katika biashara na matumizi haramu ya dawa za kulevya na silaha, kwa sasa rushwa imepenyeza mizizi yake katika masuala ya uchumi, mazingira, katika huduma za kiafya na maliasili.

Rushwa inakwamisha ukuaji chanya wa uchumi kwa kuongeza gharama za uzalishaji na vitisho; inahatarisha haki msingi za binadamu na kuongeza baa la umaskini wa hali na kipato kati ya watu wa mataifa; ni janga ambalo linachangia kukua na kupanuka kwa pengo la wenye nacho na "akina yakhe pangu pakavu, tafadhali tia mchuzi"!

Hii ni fedha na rasilimali ambayo ingechangia kuleta maboresho ya huduma za elimu, afya na maendeleo ya jamii, lakini kwa bahati mbaya zinaishia mikononi mwa watu wachache, wenye uchu wa mali na madaraka.

Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa anasema kwamba, rushwa inaendelea kusababisha majanga makubwa kwa ustawi na maendeleo ya watu duniani. Rushwa katika huduma za afya inakadiriwa kwamba, inagharimu kiasi cha dolla za kimarekani billioni 12 hadi 24 kwa Mwaka.







All the contents on this site are copyrighted ©.