2013-12-10 10:37:23

Ukisikia watu wanapiga vigelegele, hapo tambua kuna mtu anajisadakisha!


Watawa watatu wa Shirika la Mapendo, maarufu kama Rosmini, Jumatatu tarehe 9 Desemba 2013 wameweka Nadhiri za daima, kwenye Ibada ya Misa Takatifu iliyoongozwa na Padre Vito Nardin, kwenye Kanisa kuu la Giovanni Porta Latina, lililoko mjini Roma na kuhudhuriwa na idadi kubwa ya Mapadre na Watawa kutoka: India, Tanzania na Kenya.

Watawa wa Shirika la Mapendo kwa njia ya nadhiri za daima wameimarisha ndani mwao neema na baraka walizojaliwa na Roho Mtakatifu wakati wa Ubatizo, tayari kumwilisha Sheria za Warosmini katika safari ya maisha na utume wao kama Wanashirika, huku wakikumbatia Mashauri ya Kiinjili, yaani: Utii, Useja na Ufukara. Injili ya Kristo na Sheria za Shirika kwa sasa ndio mwongozo makini wa maisha yao kwa ajili ya huduma kwa Mungu na jirani.

Padre Vito Nardin katika mahubiri yake, amewapongeza watanzania waliokuwa wanaadhimisha Miaka 52 tangu walipojitwalia Uhuru wa bendera kutoka kwa Mwingereza na Wakenya wanaposherehekea Jubilee ya Miaka 50 tangu walipojipatia uhuru wao. Watawa wa Shirika la Mapendo wamekumbushwa kwamba, wanapaswa kuwa tayari kutumwa na Kristo mahali na wakati wowote na kwa maisha yao yote!

Watawa hawa wameweka nadhiri za daima baada ya kukamilisha kipindi cha majiundo na malezi mintarafu sheria, kanuni na maagizo ya Mama Kanisa. Kwa sasa wako tayari kuonesha utii kwa Mwenyezi Mungu, wakiendelea kushibishwa kwa adhimisho la Fumbo la Ekaristi Takatifu, ili kuzima kiu ya maisha ya ndani, tayari kukumbatia Mashauri ya Kiinjili.

Padre Nardin amekumbusha kwamba, maisha ya kitawa ni kielelezo cha hali ya juu cha utii kwa Mwenyezi Mungu, kwa ajili ya kutangaza Habari Njema ya Wokovu hadi miisho ya dunia. Watawa katika maisha yao ya kila siku, wanapaswa kuwa ni mashahidi wanaoleta changamoto chanya ya maisha mapya kwa ajili ya watu wa kizazi hiki kama walivyofanya Warosmini waliowatangulia katika maisha ya kitawa.

Watawa wanahimizwa kumwilisha ndani mwao, Heri za Mlimani, ambazo kimsingi ni muhtasari wa Mafundisho Makuu ya Yesu kwa wafuasi wake; tayari kuwaendea maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii ili kuwatangazia Injili ya Furaha na kuwaonjesha huruma na upendo wa Mungu, kama anavyokazia Baba Mtakatifu Francisko. Watawa wanahamasishwa na Mama Kanisa kama walivyo waamini wengine wote kujitahidi kuwa watakatifu, kwa kumfuasa Kristo aliyekuwa: Mtii, Mseja na Fukara. Kristo awe ni utambulisho wa maisha na sadaka yao ya kitawa.

Yesu ni kielelezo cha sura ya Mungu katika maisha ya mwanadamu anasema Padre Nardin katika mahubiri yake ya kwanza katika tukio kama hili tangu alipochaguliwa hivi karibuni kuliongoza Shirika la Mapendo. Watawa wanakumbushwa kwamba, maisha ya kitawa ni mwaliko wa kujisadakisha kwa ajili ya Mungu, Kanisa na Jirani. Maisha haya yawe ni mwanga unaoleta matumaini mapya mintarafu mapenzi ya Mungu kwa watu wake.

Watawa walioweka Nadhiri za daima, wametakiwa kuwa ni wachapakazi, wanyenyekevu, wavumilivu kwani katika hija ya maisha na utume wao, watakumbana na vikwazo pamoja na vizingiti, lakini hawapaswi kukata tamaa, bali wasonge mbele kwa kutambua kwamba, Mwenyezi Mungu amewaita na atawategemeza katika maisha na utume wao.

Wasikatishwe tamaa na mapungufu ya kibinadamu yanayofanywa na baadhi ya viongozi wa Shirika au Kanisa; wasaidiane kidugu, huku wakiheshimiana na kwamba, wanapaswa kujisikia kuwa ni sehemu ya Jumuiya inayojengeka katika msingi wa mapendo ya kidugu! Ushuhuda wa umoja na mshikamano, kiwe ni kikolezo, mvuto na mashiko kwa wale wanaowazunguka, katika kumfuasa Yesu Kristo.

Padre Vito Nardon amewaweka wanashirika wapya chini ya ulinzi na usimamizi wa Bikira Maria wa miito, ili awasaidie kujifunza: haki, upendo na kuyasadakisha maisha yao kwa ajili ya Mungu na jirani. Watawa walioweka nadhiri zao za daima ni: Aji Alphonce kutoka India, Aristid Shayo kutoka Tanzania na Justus Okibo kutoka Kenya.







All the contents on this site are copyrighted ©.