2013-12-10 07:51:15

Mawasiliano ya Jamii na changamoto zake!


Njia mpya za mawasiliano ya kijamii zinaendelea kuleta mabadiliko na changamoto kubwa katika Jamii. Barani Ulaya, mitandao ya kijamii imekuwa ni jukwaa maalum kwa ajili ya majiundo ya binadamu, mahali ambapo watu wanawasiliana na kushirikishana mang’amuzi ya maisha sanjari na ujenzi wa mahusiano ya kijamii, hasa miongoni mwa vijana wa kizazi kipya. RealAudioMP3

Ni jukwaa linalogusa undani wa maisha ya mwanadamu kwa kutumia lugha, mbinu mpya na zile za zamani katika kufikisha ujumbe kwa hadhira inayokusudiwa.

Hii ni fursa makini inayolihamasisha Kanisa kuhakikisha kwamba, linapeleka ujumbe wa Injili unaogusa sakafu za mioyo ya watu! Uinjilishaji mpya ni dhamana inayotekelezeka hata kwa njia ya sana na kwamba, kuna uhusiano wa karibu sana kati ya Liturujia na Uhandisi. Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican wamekuwa wakilihamasisha Kanisa kusoma alama za nyakati pamoja na kuhakikisha kwamba, linatumia maendeleo ya sayansi na teknolojia ya habari katika azma ya Uinjilishaji Mpya.

Baba Mtakatifu Francisko ameendelea kuonesha umuhimu wa matumizi ya mitandao ya kijamii katika mchakato wa Uinjilishaji Mpya. Hadi sasa anazaidi ya wafuasi millioni kumi katika akaunti yake ya twitter. Hii inaonesha kwamba, Kanisa linaweza kujikita katika Uinjilishaji Mpya hata kwa kutumia mitandao ya kijamii. Mama Kanisa anapofanya kumbu kumbu ya Miaka 50 tangu Hati ya Kichungaji kuhusu Vyombo vya Mawasiliano ya Kijamii, Inter Mirifica ilipotolewa kwa mara ya kwanza na Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican, Kanisa bado lina changamotishwa kusoma alama za nyakati sanjari na matumizi sahihi ya vyombo hivi kwa kuzingatia: sheria, kanuni, utu na maadili mema.

Haya ni kati ya mambo msingi yaliyojadiliwa na wajumbe Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Ulaya, katika mkutano wa Maaskofu wenye dhamana ya vyombo vya habari kutoka katika Mabaraza husika. Mkutano huu uliofanyika mjini Barcelona, umeongozwa na kauli mbiu “uinjilishaji wa roho za waamini Barani Ulaya”. Wajumbe wamepembua changamoto zinazolikabili Kanisa katika utekelezaji wa dhamana yake ya Umissionari; mchakato wa mawasiliano unaofanywa na Baba Mtakatifu Francisko, kiasi cha kuwagusa watu wengi pamoja na teknolojia mpya za mawasiliano ya kijamii.

Waamini wanaalikwa kwa namna ya pekee kuona ukuu na matendo ya Mungu kwa njia ya sanaa ya uhandisi, jambo linaloonesha ushuhuda wa mwamini aliyefanya tafakari ya kina kwa kukutana na Yesu, kama anavyokazia Baba Mtakatifu Francisko. Matumizi ya njia mpya za mawasiliano ni kati ya mambo yaliyosababisha mabadiliko makubwa katika maisha na utume wa Majimbo kadhaa Barani Ulaya, kama ilivyo jidhihirisha katika Jimbo kuu la Barcelona. Mambo yote haya yamejadiliwa kwa kina ili kulisaidia Kanisa kutoa majibu makini katika kukabiliana na changamoto hizi.

Askofu mkuu Claudio Maria Celli, Rais wa Baraza la Kipapa la Mawasiliano ya Jamii anasema, Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican walikazia kwa namna ya pekee usomaji wa alama za nyakati kwa kuendelea kutumia njia za mawasiliano ya Kijamii kwa ajili ya Uinjilishaji. Wakati huu Mama Kanisa hana budi kujikita pia katika matumizi ya mitandao ya kijamii ili kuhakikisha kwamba, ujumbe wa Habari Njema ya Wokovu unawafikia watu mahali walipo!

Anasema, Mama Kanisa hakutumwa kuinjilisha mitandao, bali kuinjilisha kwa njia ya mitandao, yaani kuwatangazia watu wanaoishi katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia kwa kutumia lugha na nyenzo bora ili kuwafikia watu wengi zaidi. Huu ni ujumbe unaopaswa kumwilishwa kwa njia ya maneno yanayojidhihirisha katika matendo, kwa maneno mengine, hii ndiyo imani tendaji.

Mitandao ya kijamii ikitumiwa vyema inaweza kusaidia kuhamasisha kundi kubwa la watu, ili kuwa na mwelekeo na sera makini zaidi zinazozingatia ut una heshima ya binadamu. Mitandao ya kijamii imetumika nchini Ufaransa kuhamasisha waamini na watu wenye mapenzi mema, kusimama kidete kupinga ndoa za watu wa jinsia moja kwani zinakwenda kinyume cha mapenzi ya Mungu na utu wema. Mafanikio makubwa yamejionesha kwa namna ya pekee nchini Ufaransa.

Kanisa halina budi kutumia njia za mawasiliano kadiri ya mapokeo pamoja na njia za kisasa, ili kuwagusa watu wengi zaidi, kadiri ya mahitaji ya hadhira inayokusudiwa. Baba Mtakatifu katika uongozi wake tangu alipochaguliwa ameonesha jinsi ya kuwasiliana katika uhalisia wa maisha pasi na “mkwara” na kwamba, ujumbe wa Kikristo unaosimikwa katika mapendo kwa Mungu na jirani, unaendelea kuwagusa watu wengi zaidi.

Baba Mtakatifu anafundisha Injili ambayo ameifanyia tafakari ya kina na anapenda kuimwilisha kwa njia ya matendo. Ni kiongozi anayependa kuzungumza na mtu mmoja mmoja na wala si makundi ya watu! Anapenda kumwita mtu kwa jina! Mwishoni, wajumbe wameshauri kwamba, Maaskofu wenye dhamana ya kusimamia vyombo vya upashanaji habari wanapaswa kukutana mara kwa mara, ili kuimarishana na kubadilishana uzoefu na mang’amuzi tayari kupambana na changamoto zinazojitokeza katika ulimwengu wa mawasiliano ya kijamii.








All the contents on this site are copyrighted ©.