Kanisa la Waadventisti lazindua Jimbo kuu Kusini mwa Tanzania
Waziri mkuu wa Tanzania Mizengo Pinda amewataka Watanzania waendelee kuombea amani,
ustawi na maendeleo ya Taifa zima bila kujali tofauti zao za dini na kusisitiza kwamba
kila mmoja ana wajibu wa kutunza amani iliyopo. Ametoa wito huo Jumamosi, Desemba
7, 2013 wakati akizindua Jimbo Kuu la Kusini mwa Tanzania (Southern Tanzania Union
Mission) la Kanisa la Waadventista Wasabato kwenye sherehe zilizofanyika kwenye Viwanja
vya Mwalimu J. K. Nyerere, barabara ya Kilwa jijini Dar es Salaam. Akizungumza
na waumini zaidi ya 13,000 wa Kanisa hilo walioshiriki uzinduzi huo, Waziri Mkuu alisema:
“Mtu asiyejua vurugu hawezi kujua thamani ya amani... lakini lazima tujue madhara
ya vurugu huwa ni makubwa kwa watoto, wanawake na wazee.” Aliwasihi viongozi wa kanisa
hilo pamoja na waumini kuendelea kuliombea Taifa pamoja na Watanzania wote. “Mimi
huwa nafarijika sana ninaposikia sehemu fulani kuna maombi kwa ajili ya Taifa, kwa
hiyo ninawaomba Maaskofu na waumini msichoke kuliombea Taifa letu,” alisema. Mbali
na kuliombea Taifa pamoja na kuwaombea waamini wake, Waziri Mkuu aliwataka viongozi
wa Kanisa kuendelea kushirikiana na Serikali kutafuta njia ya kuwasaidia waamini wake
kukua kiuchumi. “Kanisa lina wajibu wa kuwasaidia wananchi kukua kiuchumi na mimi
natambua waamini wa Kanisa hili ni wakulima na wafugaji ama vyote viwili.” Waziri
Mkuu alisema moja ya kazi kubwa ya kanisa ni kusaidia waumini wake kukua kiroho na
kimwili. Lakini kanisa pia linahitaji kuona maisha ya waumini yanakuwa bora zaidi.
”Tunategemea uchumi wa muumini mmoja mmoja kukua na hivyo uchumi wa kanisa, na uchumi
wa Taifa kwa ujumla kukua,” aliongeza. Alisema anataraji kwamba kupatikana kwa
Jimbo Kuu la Kusini kutakuwa ni chachu ya kupata maendeleo zaidi ya kiuchumi katika
Jimbo hilo ambalo linafaa sana kwa kilimo. “Pia, tunategemea kasi ya kupata waumini
wapya itaongezeka kutokana na kugawanywa kwa Jimbo Kuu moja na kuwa Majimbo Makuu
mawili, hivyo kusogeza huduma za kiroho na kiuchumi karibu zaidi na waamini,” alisema. Waziri
Mkuu alisema Jimbo Kuu la Kusini lililozinduliwa jana linajumuisha mikoa ambayo ni
maarufu kwa shughuli za kiuchumi. “Imetajwa mikoa takriban 11 ya Tanzania Bara na
Mitano ya Visiwani. Ipo mikoa ya Dar es Salaam, Dodoma, Iringa, Katavi, Lindi na Mbeya.
Mikoa mingine ni Morogoro, Mtwara, Pwani, Rukwa na Ruvuma. Hakika ni eneo kubwa la
kuongoza.” “Kinachotakiwa ni kwa Kanisa kujipanga vizuri kwa kujiwekea mikakati
ya maendeleo. Nawaombeni sana kuanzia sasa, tuwahimize waumini wetu hasa vijana wajikite
pia katika kuanzisha miradi ya kilimo na ufugaji, ikiwemo kilimo cha mazao na ufugaji
nyuki. Mkitumia fursa hizi zinazowazunguka katika maeneo yetu ya Jimbo hili, mnaweza
kabisa kuleta ukombozi wa kiuchumi, hususan kwa vijana wetu,” alisisitiza.
Kanisa
hilo lenye waumini wapatao milioni 17.2 duniani, lina makao yake makuu nchini Marekani.
Hapa Tanzania lina waumini milioni tano na lilikuwa na jimbo kuu moja ambalo liligawanywa
katika majimbo sita na makao yake makuu kwenye mabano kama ifuatavyo:- Kaskazini Mashariki
(Same), Kusini mwa Ziwa Victoria (Mwanza), Mara (Musoma), Mashariki (Morogoro), Nyanda
za Juu Kusini (Mbeya) na Magharibi (Kigoma). Mapema, akisoma risala mbele ya Waziri
Mkuu, Katibu Mkuu wa Jimbo Kuu la Kusini, Mchungaji James Machage alisema kutokana
na kupanuka kwa kazi, kanisa hilo limeona vema hapa nchini kuwe na majimbo makuu mawili
badala ya moja. Alisema Jimbo Kuu la Kaskazini ambalo makao yake makuu yatakuwa Arusha
litahusisha majimbo ya Mara, Kusini mwa Ziwa Victoria, Magharibi na Kaskazini Mashariki
wakati Jimbo Kuu la Kusini litahusisha majimbo ya Mashariki na Nyanda za Juu Kusini
na makao yake makuu yatakuwa Jijini Dar es Salaam.