2013-12-09 10:48:24

Dunia inamkumbuka Tata Madiba! RIP.


Afrika ya Kusini, Jumapili iliyopita imetumia siku hii kwa ajili ya kusali, kufunga na kutafakari kuhusu mchango wa Mzee Nelson Mandela, enzi ya uhai wake. Wananchi wa dini na madhehebu mbali mbali wameungana kusali ili kumwombea Tata Madiba pamoja na kuliombea Taifa la Afrika ya Kusini, linapoanza awamu mpya baada ya kifo cha Mzee Madiba.

Rais Jacob Zuma anasema, Mzee Madiba alijipambua kwa tunu msingi za maisha ya kiutu, ni kama mwanga uliotumwa kufukuza giza na vivuli vilivyokuwa vinamsonga mwanadamu. Aliwapatia watu wake matumaini makubwa na akawatengenezea maisha kwa leo na kesho iliyo bora zaidi. Alionesha moyo wa kusamehe na kusahau; alikuwa ni mtu wa haki na ukarimu kwa jirani zake; alisimama kidete kulinda na kutetea zawadi ya uhai.

Bwana Josè Graziano da Silva, Mkurugenzi mkuu wa Shirika la Kilimo na Chakula la Umoja wa Mataifa, FAO anamkumbuka Mzee Mandela, kwa kusimama kidete dhibi ya baa la njaa na umaskini duniani, kama kielelezo cha uhuru wa kweli kwa binadamu. Akawataka wakuu wa Jumuiya ya Kimataifa kutunga sera makini katika mapambano dhidi ya baa la njaa na umaskini. Hata leo hii kuna watu millioni 842 ambao wanakabiliwa na baa la njaa duniani.

Shirika la Wakimbizi la Umoja wa Mataifa linasema kwamba, Mzee Madiba alionesha ushirikiano wa hali ya juu katika kukabiliana na tatizo la wakimbizi duniani. Aliguswa na hali ya wakimbizi kutoka Afrika ya Kusini, waliokuwa wamelazimika kuikimbia nchi yao kutokana na utawala wa ubaguzi wa rangi Afrika ya Kusini, enzi hizo.

Ni kielelezo cha mwanasiama mahiri aliyetambua na kuonja shida za wahamiaji, ambao hata leo hii wanalazimika kuzikimbia nchi zao kutokana na vita, kinzani, majanga asilia pamoja na kutafuta fursa za ajira.

Bwana Anthony Lake, Mkurugenzi mkuu wa Shirika la kuhudumia Watoto la Umoja wa Mataifa, UNICEF anasema kwamba, tangu mwaka 2002 Mzee Madiba alijitoa mhanga kwa ajili ya kampeni ya kuwasaidia watoto kupata haki yao msingi ya elimu. Watoto millioni mbili kutoka Barani Afrika wakabahatika kupata fursa ya kwenda shule. Alishirikiana kwa karibu sana na UNICEF ili kuhakikisha kwamba, elimu kwa watoto wadogo inakuwa ni sehemu ya ajenda za maendeleo kwa Jumuiya ya Kimataifa.







All the contents on this site are copyrighted ©.