2013-12-07 15:31:47

Uwepo wa Kanisa katika mitandao ya kijamii ni kuwaonjesha watu huruma ya Mungu inayofunuliwa kwa njia ya Neno wa Mungu aliyefanyika mwili!


Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican umewapatia nafasi waamini walei kuweza kuchangia katika ustawi, maisha na utume wa Kanisa kwa kutambua kwamba, wanatumwa ulimwenguni ili kuweza kuyatakatifuza malimwengu.

Hizi ndizo juhudi zilizofanywa na Baraza la Kipapa kwa ajili ya Walei katika Maadhimisho ya Kongamano la Waamini Walei Barani Afrika lililofanyika kunako Mwaka 2012; nafasi ya wanawake, kama sehemu ya Maadhimisho ya Jubilee ya Miaka 25 tangu Mwenyeheri Yohane Paulo II alipochapisha Waraka juu ya Heshima ya Wanawake, Mulieris Dignitatem. Katika ulimwengu wa utandawazi, wanawake wanapaswa kua mstari wa mbele katika kumlinda mwanadamu.

Kanisa limeendelea pia kuwekeza katika majiundo makini kwa vijana, katika Maadhimisho ya Siku za Vijana Duniani kama ilivyotokea mjini Rio de Janeiro, Brazil. Vijana wamehamsishwa kuendeleza asili na dhamana ya Kanisa ambalo kimsingi ni la Kimissionari, ili kutangaza Injili ya Furaha kwa watu wa mataifa, baada ya kukutana na Yesu Kristo katika hija ya maisha yao ya kiroho, ili waweze kuleta mabadiliko na matumaini ya maisha kwa jirani zao!

Ni maneno ya Baba Mtakatifu Francisko, wakati alipokutana na kuzungumza na Wajumbe wa Baraza la Kipapa kwa ajili ya Walei, waliokuwa na mkutano wao wa Mwaka kuanzia tarehe 5 hadi tarehe 7 Desemba 2013, kwa kuongozwa na tema "Kumtangaza Kristo nyakati za Dijitali".

Mitandao ya kijamii anasema Baba Mtakatifu ni jukwaa muhimu sana la Uinjilishaji miongoni mwa vijana. Maendeleo ya mitandao ya kijamii yanahitaji kwa namna ya pekee kuweka uwiano bayana kati ya imani na utamaduni. Kanisa limeendelea kutumia tamaduni mbali mbali ili kuwatangazia Watu wa Mataifa Habari Njema ya Wokovu, tangu wakati wa Wagriki.

Kanisa likajifunza Falsafa na mbinu za elimu, lakini likawa huru kutupilia mbali mambo ambayo yalikuwa yanasigana na imani; na tamaduni nyingi zikaguswa na kweli za Kiinjili, kwa kuchukua tunu bora na kuacha makapi! Hivi ndivyo ilivyo pia hata katika matumizi ya mitandao ya kijamii, kuna mambo mazuri yanayopaswa kuchukuliwa na kuenziwa na Mama Kanisa, lakini pia kuna hatari zinazopaswa kuepukwa. Kwa kuongozwa na Roho Mtakatifu waamini wanaweza kung'amua fursa zinazopatikana katika mchakato wa kuutafuta uso angavu wa Kristo.

Baba Mtakatifu anasema, hili ni jukwaa makini la Uinjilishaji, ingawa haitoshi kuwa na teknolojia tu, bali kujenga na kudumisha mchakato utakaowawezesha watu kukutana; hawa ni wale ambao wamepoteza dira na njia; watu ambao wamejeruhiwa; ili waweze kuonjeshwa matumaini mapya.

Utangazaji wa Injili unahitaji watu kujenga na kudumisha uhusiano wa dhati na Kristo na kwamba, uwepo wa Kanisa katika mitandao ya kijamii ni muhimu sana. Hapa ni maskani ya maisha ya vijana, wanaopaswa kusaidiwa ili kuamsha ndani mwao maana ya maisha kwa kuwaonjesha huruma ya Mungu inayojifunua kwa njia ya Yesu Kristo, Neno wa Mungu aliyefanyika mwili!







All the contents on this site are copyrighted ©.