Tume ya Kipapa kwa ajili ya kulinda na kuwatetea watoto kuanzishwa hivi karibuni!
Baba Mtakatifu Francisko ameamua kuanzisha tume maalum ya kipapa itakayoshughulikia
masuala ya kuwalinda watoto dhidi ya nyanyaso za kijinsia na itakuwa na dhamana ya
kumshauri mambo muhimu ambayo Kanisa linapaswa kuyatekeleza katika mikakati yake ya
kichungaji kwa ajili ya usalama na ustawi wa watoto.
Hayo yamebainishwa na
Kardinali Sean Patrick O'Malley, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Boston, Marekani ambaye
pia ni mjumbe wa Tume maalum ya Makardinali wanane iliyoundwa na Baba Mtakatifu Francisko
ili kumsaidia kupata ushauri wa kufanya mageuzi ndani ya Kanisa. Tume hii imehitimisha
kikao chake cha pili, ambacho Baba Mtakatifu Francisko ameshiriki pia. Uamuzi huu
ni mwendelezo wa hatua madhubuti zilizokuwa zimeanza kuchukuliwa na Baba Mtakatifu
mstaafu Benedikto wa kumi na sita katika mchakato wa kupambana na nyanyaso za kijinsia
zilizokuwa zinafanywa na baadhi ya viongozi wa Kanisa.
Tume itakuwa inamjulisha
mara kwa mara Baba Mtakatifu na hatua ambazo Baraza ya Kipapa kwa kushirikiana na
Mabaraza ya Maaskofu Katoliki pamoja na Mashirikisho ya Wakuu wa Mashirika ya Kitawa
na Kazi za kitume wanayopaswa kuchukua. Tume hii itawashirikisha: Walei, Watawa na
Mapadre, watakaokuwa na dhamana ya kulinda na kutetea utu na heshima ya watoto; kujenga
uhusiano wa karibu na waathirika pamoja na kuwasaidia kupata tiba muafaka na utekelezaji
wa sheria husika. Tume hii itatangazwa na Baba Mtakatifu ikiambatana na Hati maalum
ya shughuli za kichungaji.
Kwa upande wake, Padre Federico Lombardi, msemaji
mkuu wa Vatican amebainisha kwamba, mkutano wa Tume ya Makardinali awamu ya pili umehitimishwa
kwa ushiriki wa Baba Mtakatifu Francisko. Mkutano mwingine wa Makardinali hao wanane
utafanyika tena kuanzia tarehe 17 hadi tarehe 19 Februari 2014. Kutafuatia Baraza
la Makardinali litakaloanza kikao chake tarehe 20 hadi 21 Februari 2014 na Makardinali
wapya watatangazwa hapo tarehe 22 Februari, wakati wa Maadhimisho ya Siku kuu ya Ukulu
wa Mtakatifu Petro na Jumapili tarehe 23 Februari 2014, Makardinali wapya wataadhimisha
kwa pamoja Fumbo la Ekaristi Takatifu, kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini
Vatican.
Padre Lombardi anasema, tarehe 24 hadi 25 Februari 2014, Sekretarieti
kuu ya Sinodi ya Maaskofu itakuwa na kikao chake hapa mjini Vatican, kama sehemu ya
maandalizi ya Maadhimisho ya Sinodi ya Maalum ya Maaskofu kwa ajili ya Familia, itakayofanyika
mjini Vatican mwezi Oktoba, 2014.