2013-12-06 10:47:34

Tata Madiba alijisadakisha kwa ajili ya utu na heshima ya binadamu!


Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Bwana Ban Ki-Moon anasema amepokea kwa majonzi makubwa habari za kifo cha Mzee Madiba, Nelson Mandela, Rais mstaafu wa Afrika ya Kusini, aliyesimama kidete kutetea haki msingi za binadamu; mfungwa wa dhamiri, ambaye kamwe hakulalamika hata baada ya kukosewa haki zake msingi; alikuwa ni mtetezi wa haki kimataifa, Rais wa kwanza mzalendo na mfano wa kuigwa na wengi!

Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa, kwa niaba ya Umoja wa Mataifa anapenda kutuma salam zake za rambi rambi kwa wananchi wa Afrika ya Kusini na kwa namna ya pekee kwa familia yake. Watu wengi duniani waliguswa na kuhamasishwa na sadaka kubwa iliyotolewa na Mzee Madiba katika kulinda na kutetea: utu, heshima, usawa na uhuru wa kweli. Ni mfano wa pekee katika Jumuiya ya Kimataifa katika kutetea mafao ya wengi kwa ari na moyo mkuu.

Bwana Ban Ki-Moon anasema, Mzee Madiba ameonesha kwamba, inawezekana watu kufanya kazi kwa umoja, upendo na mshikamano wa dhati kwa ajili haki na utu wa mwanadamu. Kanuni maadili ilimsukuma kupinga vitendo vyote vya ubaguzi wa rangi na baada ya kuporomoka kwa utawala wa ubaguzi wa rangi, akaanzisha mchakato wa majadiliano, haki na amani; ukweli na uptanisho.

Ni kiongozi aliyejisadaka kwa ajili ya haki msingi za binadamu, mchango ambao wengi wameshiriki hata bila kujitambua kama alivyosema Tata Madiba alipokutana na Bwana Ban Ki-Moon siku moja!







All the contents on this site are copyrighted ©.