2013-12-06 08:29:25

Tafakari ya Neno la Mungu, Jumapili ya Pili ya Kipindi cha Majilio


Tunaendelea katika kushirikishana meza ya Neno la Mungu, tayari tukiwa katika Dominika ya II ya Majilio mwaka A. RealAudioMP3

Neno la Mungu ndiyo dira na taa ya maisha yetu. Mwaliko wa Neno la Mungu Dominika iliyopita ulikuwa ni kukesha na kusali kwa maana hatujui siku wala saa atakayokuja Bwana wetu, na Dominika hii tunaalikwa KUTAYARISHA NJIA YA BWANA.

Katika mantiki ya kutayarisha njia ya Bwana yatupasa kufikiri kwa nini tunaalikwa kufanya hivyo? Tunaalikwa kutenda hivyo kwa sababu Masiha ajaye ni kiongozi na mfalme wa mbingu na dunia, kumbe hatuna budi kumkaribisha. Huyu kiongozi ajaye, katika somo la I anajulikana kama tawi litakalochipuka katika shina la Yese. Sifa yake ya pekee, anayo hekima na ufahamu wa pekee kwa ajili ya kazi yake ya wokovu.

Mpendwa mwana wa Mungu, ujumbe wa kutayarisha njia ya Bwana, unaletwa kwetu na Nabii Yohane Mbatizaji ambaye anatoa sauti ya kutangaza akiwa jangwani. Mwaliko wa Yohane Mbatizaji uko katika TOBA kwa ajili ya kutayarisha mioyo yetu ili kumpokea Mungu. Yohane Mbatizaji anapotangaza ujumbe huu anaturudisha nyuma kidogo katika maneno ya Nabii Isaya anayeishi katika karne ya 8 hivi kabla ya Kristu asemaye: sauti ya mtu aliaye nyikani, itengenezeni njia ya Bwana, yanyosheni mapito yake.

Ndiyo kusema Yohane Mbatizaji anakazia na kuyaweka katika matendo mausia ya Mungu kwa njia ya Nabii Isaya. Yohane anataka watu wafunge na kwa njia hiyo wafungue mioyo yao tayari kwa wokovu. Anakazia kuwa wokovu hauji kwa njia ya miujiza bali lazima mmoja aongoke na kuifuata njia ya Bwana. Anataka watu waungame dhambi zao, kama ambavyo twafahamu jinsi walivyomwendea watu wa zama hizo pale katika mto Yordani.

Mpendwa msikilizaji, mwaliko wa Yohane Mbatizaji katika majilio haya ni toba inayogeuza maisha yetu kwa dhati kabisa bila kurudi nyuma. Toba anayoidai Yohane ni ile inayokuza jina la Bwana kwa njia ya unyenyekevu, kama yeye alivyotangaza wazi kuwa yeye hasitahili kugusa hata kamba za viatu vya Bwana ajaye yaani Masiha.

Katika somo la pili Mtume Paulo anaweka sala kwa ajili yetu akisema “Mungu awajalieni kuwa na msimamo mmoja kufuatana na mfano wake Kristu Yesu. Msimamo wake Yesu uwe msimamo wetu na zaidi ya yote fadhila ya upendo kwa watu ikomae. Kumbe kutayarisha njia ya Bwana ni katika kueneza upendo kwa watu wa Mungu. Kila mmoja anayejaribu kuweka maisha yake kwa ajili ya wengine anakuwa Kristu mwingine aliyejitoa maisha yake kwa ajili ya ulimwengu.

Basi mpendwa msikilizaji, jiwekeni daima katika usikivu ili maneno ya Yohane Mbatizaji na Mt. Paulo yawe chakula chako cha kila siku na hiyo ndiyo namna ya kuishi majilio ukitayarisha njia ya Bwana.

Nikutakie Dominika njema na majilio njema katika kujiweka tayari kwa kuzaliwa Mtoto Emanueli. Tumsifu Yesu Kristo na Bikira Maria.

Tafakari hii imeletwa kwako na Pd Richard Tiganya, C.PP.S.








All the contents on this site are copyrighted ©.