Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Mrisho Kikwete amemtumia Salamu za
rambirambi Rais Jacob Zuma wa Afrika ya Kusini na kupitia kwake, kwa mkewe Bi. Graca
Machel, wanafamilia wote na wananchi wote wa Afrika ya Kusini kufuatia kifo cha Mzee
Nelson Mandela kilichotokea tarehe 5 Desemba, 2013 baada ya kuugua kwa muda mrefu. Rais
ameuelezea msiba huu kuwa ni msiba mkubwa kwetu sote. "Afrika ya Kusini, Afrika
na dunia kwa ujumla imepoteza mtu mashuhuri na shujaa mkubwa wa Karne ya 20 na 21.Tunaelewa
machungu waliyonayo wananchi wa Afrika ya Kusini kwa kupoteza kiongozi shupavu, jasiri,
mwana mapinduzi , mvumilivu na mstahimilivu". Ameongeza Rais Kikwete.
Rais
amemuelezea Mzee Mandela kuwa ni kielelezo cha aina yake kwa wanadamu kwa moyo wake
wa kusamehe, huruma na upendo uliomuwezesha kuwaunganisha wananchi wa Afrika ya Kusini
kuwa taifa moja baada ya kipindi kirefu cha mapambano dhidi ya ubaguzi wa rangi.
"Mandela
ni mfano bora kwa wanadamu wa jinsi binadamu muungwana anavyopaswa kuwa . Ni wajibu
wa wana Afrika Kusini, Afrika na dunia kwa jumla kuiga mfano wake hasa moyo wake wa
uzalendo, kujitolea hata maisha yake kwa ajili yake na wananchi wenzake" .Rais ameongeza
kusema, "Tuzidi kumuombea kwa Mwenyezi Mungu ailaze roho ya Marehemu Mzee Mandela
mahali pema peponi". Kufuatia kifo hicho Rais ametangaza siku 3 za maombolezo kuanzia
leo tarehe 6 hadi 8 Desemba, 2013. Aidha, Mheshimiwa Rais ameagiza kuwa katika siku
hizo 3 bendera zote zipepee nusu mlingoti.